Chanzo cha picha, Getty Images
-
- Author, Simon Casson
- Nafasi, BBC Sport senior journalist
-
Ousmane Dembele mchezaji bora wa dunia mwaka huu akitwaa tuzo ya Ballon d’Or Jumatatu hii. Lakini wako nyota wakali zaidi kuwahi kutokea ambao hawajawahi kutwaa tuzo hiyo. Majina yanayotajwa ni kama orodha ya wakubwa wa soka duniani: Neymar, Kylian Mbappé, Robert Lewandowski, Thierry Henry, Dennis Bergkamp, Andrés Iniesta, David Beckham…
Wote hawa wamekuwa na kazi za kupigiwa mfano na kushinda makombe lukuki, lakini kuna kitu kimoja wanachoshirikiana hakuna hata mmoja wao aliyewahi kushinda Ballon d’Or kwa upande wa wanaume.
Tuzo hii ya kifahari hupewa kila mwaka tangu 1956, ilipoanzishwa na waandishi wa michezo kutoka Ufaransa kutambua vipaji bora vya dunia.
Awali ilikuwa kwa wachezaji wa Ulaya pekee, lakini sasa inatolewa kwa wanasoka kutoka pande zote za dunia.
Katika orodha ya washindi kuna majina makubwa kama Zinedine Zidane, Ronaldinho na Ronaldo wa Brazil. Lakini tangu 2008 kulikuwa na enzi ya utawala wa Lionel Messi na Cristiano Ronaldo wakibadilishana tuzo hii kwa miaka zaidi ya kumi.
Swali kubwa sasa ni: ni akina nani mastaa wakubwa waliokosa kabisa kushinda Ballon d’Or?
Chanzo cha picha, Getty Images
Dennis Bergkamp
Anahesabiwa kama mmoja wa vipaji vikubwa zaidi kizazi chake. Arsenal ilimnunua mwaka 1995 kutoka Inter Milan kwa £7.5m – na ikawa biashara bora kabisa.
Alishinda mataji matatu ya ligi, ikiwemo lile la “Invincibles” mwaka 2003-04, pamoja na Kombe la FA mara tatu.
Goli lake la kipekee dhidi ya Argentina kwenye Kombe la Dunia 1998 linabaki historia. Hata hivyo, nafasi zake bora kwenye kura za Ballon d’Or zilikuwa 1992 (nafasi ya tatu) na 1993 (nafasi ya pili).
Chanzo cha picha, Getty Images
Thierry Henry
Mmoja wa magwiji wa Arsenal angekuwa miongoni mwa wachezaji bora kuwahi kutokea katika historia ya Ligi Kuu ya England.
Baada ya kusajiliwa na ‘The Gunners’ mnamo 1999, Thierry Henry punde tu aligeuka kuwa mmoja wa washambuliaji hatari zaidi barani Ulaya, akiwa na rekodi ya mabao inayothibitisha hilo.
Alikuwa mchezaji wa kwanza katika karne hii kufunga angalau mabao 20 na kutoa pasi za mabao (assist) 20 katika msimu mmoja kwenye ligi tano kuu za Ulaya. Ni Lionel Messi pekee ndiye aliyefikia rekodi hiyo baadaye kwenye ligi za nyumbani.
Mfaransa huyo bado anashikilia rekodi ya ufungaji bora wa muda wote wa Arsenal, akiwa na mabao 228 katika mechi 377. Alipokea tuzo nyingi za kutambua mchango wake, lakini nafasi yake ya juu zaidi katika kinyang’anyiro cha tuzo ya Ballon d’Or ilikuwa kumaliza katika nafasi tatu za juu mara mbili.
Chanzo cha picha, Getty Images
Neymar
Mfungaji bora wa muda wote wa Brazil, zaidi ya mabao 400 katika kazi yake.
Kama hiyo haitoshi, yeye pia ni mmoja wa wachezaji watano pekee waliowahi kufunga mabao 100 na vilabu vitatu tofauti: Santos, Barcelona, na Paris St-Germain.
Cristiano Ronaldo, Robert Lewandowski, Romario, na gwiji wa Hispania, Isidro Langara, ndio wengine waliofanikisha rekodi hiyo.
PSG ilimsajili kwa rekodi ya dunia ya pauni milioni 200 kumsajili Neymar mwaka 2017.
Licha ya kipaji chake kikubwa na uhamisho wa rekodi ya dunia, hajawahi kushinda Ballon d’Or.
Kylian Mbappé
Chanzo cha picha, Getty Images
Katika uga wa Kimataifa, yuko na watu maarufu sana. Mbappe alikuwa kinda wa pili, akifuata nyayo za Pele, kufunga bao katika fainali ya Kombe la Dunia wakati Ufaransa walipotwaa kombe hilo mwaka 2018.
Rekodi yake ya klabu pia ni ya kushangaza sana.
Baada ya kuwa mfungaji bora wa Ligue 1 kwa misimu sita mfululizo akiwa na PSG, Mbappe amejipatia umaarufu zaidi huko Real Madrid.
Hakupoteza muda kwani alivunja rekodi ya klabu kwa mabao mengi zaidi katika msimu wa kwanza.
Robert Lewandowski
Mabao 55 msimu wa 2019/20 yalimfanya apigiwe chapuo kama mshindi wa Ballon d’Or – lakini janga la Covid lilipelekea tuzo hiyo kufutwa mwaka huo.
Mwaka uliofuata, alimaliza nafasi ya pili nyuma ya Messi.
Chanzo cha picha, Getty Images
Erling Haaland
Kiwango cha Erling Haaland katika klabu ya Manchester City ni cha ajabu. Kwa kasi yake ya ufungaji, rekodi ya Alan Shearer ya mabao 260 katika Ligi Kuu ya England inaweza kuwa hatarini, ingawa bado anahitaji mabao 169.
Haaland ameweka alama yake pia barani Ulaya. Mnorway huyu alifikisha mabao 50 katika Ligi ya Mabingwa Ulaya kwa mechi 49 tu, akawa mchezaji wa kwanza kufungfa mabao hayo kwa haraka zaidi.
Je, anaweza kuipiku rekodi ya muda wote ya Cristiano Ronaldo ya mabao 141 katika mashindano hayo?
Licha ya yote, ikiwa ataendelea kufunga kwa kasi hii, Haaland ataendelea kuwa miongoni mwa wagombea wa tuzo ya Ballon d’Or katika miaka ijayo. Hajawahi kupata tuzo hii lakini tayari ameshakuwa mshindi wa pili wa Ballon d’Or lakini
Chanzo cha picha, Getty Images
Andres Iniesta
Chanzo cha picha, Getty Images
Kama ingekuwa si kwa viwango vya ajabu walivyokuwa wakionyesha Messi na Ronaldo wiki baada ya wiki, basi kiungo mahiri Andres Iniesta labda angekuwa na tuzo ya Ballon d’Or kwenye kabati lake.
Baada ya kupita kwenye kituo cha watoto cha Barcelona cha La Masia, Iniesta alikaa vizuri kwenye safu ya kiungo ya klabu hiyo na kushinda mataji 32 katika miaka 16 yenye mafanikio makubwa, ikiwemo mataji tisa ya La Liga na manne ya Ligi ya Mabingwa.
Katika ngazi ya kimataifa, Iniesta aliichezea Hispania mechi 131 na kufunga mabao 13, ikiwemo lile la ushindi dhidi ya Uholanzi kwenye fainali ya Kombe la Dunia mwaka 2010.
Alimaliza maisha yake ya soka ya kimataifa akiwa ameshinda Kombe la Dunia mara moja na mataji mawili ya Ubingwa wa Ulaya.
Iniesta alimaliza wa pili katika kura za Ballon d’Or mwaka 2010 na wa tatu miaka miwili baadaye, wakati Messi alishinda zote mbili.