Unajua kuwa hati ya kwanza ya kusafiria ya Raila Odinga ilitolewa jijini Dar es Salaam mwaka 1962 katika nchi iliyofahamika kama Tanganyika?
Ni hati hiyo hiyo, iliyotumiwa na Waziri Mkuu huyo wa zamani wa Kenya kuingia Ujerumani Mashariki kwa ajili ya masomo yake ya elimu ya juu.
Pasipoti hiyo ya muda ilitolewa kwa Raila na vijana wengine wawili, kabla ya Tanganyika kuungana na Zanzibar mwaka 1964 na kuzaliwa Tanzania.
Kulingana na Raila mwenyewe, hii ilitokana na kwamba idara ya uhamiaji ya Kenya ambayo ilikuwa chini ya Uingereza kwa wakati huo, kumnyima hati ya muhimu, na badala yake, Waziri Mkuu wa Tanganyika kwa wakati huo, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, ambaye alikuwa swahiba wa baba mzazi wa Raila, Jaramogi Oginga Odinga, kumpatia pasipoti hiyo kutoka Tanganyika.
Hii ni kwa mujibu wa simulizi inayopatikana katika kitabu chake cha ‘The Flame of Freedom’ kilichozinduliwa mwaka 2013.
Raila, ambaye alikuwa na umri wa miaka 17, wakati huo akiwa kidato cha pili, alitakiwa aende kusoma nje ya nchi, kutokana na mahusiano mazuri kati ya Jaramogi Odinga na nchi za Umoja wa Kisoveti, tofauti na ilivyokuwa kwa serikali ya Uingereza.
Kwa upande wake, kaka yake mkubwa, Oburu Odinga ambaye alikuwa ameshatangulia kuelekea kwenye umoja wa nchi za Kisovieti, hakunyimwa tu fursa ya kujiunga na shule nzuri za Kenya, bali pia alinyimwa pasipoti ya kumwezesha kwenda nje ya nchi.
“Ombi la Oburu lilikataliwa mapema kabisa, kwa kisingizio kwamba pasipoti ya Jaramogi ilikuwa ikishikiliwa na serikali kwa sababu alikuwa ametembelea nchi za Kisoveiti na China. Kwa wakati huo, Jaramogi alikuwa akitumia pasipoti za kimataifa alizopewa na Kwame Nkrumah na Gamal Abdiel Nasser,” anasema Raila katika kitabu hicho.
Anaongeza: Katika kipindi hicho, Jaramogi alijua kwamba ili tupate elimu nzuri, basi ilitupasa tukasome nje ya nchi.