Mwili wa mwanasiasa mkongwe nchini Kenya Raila Odinga, umewasili huko Bondo karibu na kaunti ya Siaya tayari kwa mazishi ya faragha yatakayofanyika siku ya Jumapili. Kabla ya kufikishwa Bondo, mwili wa Odinga uliagwa na umati mkubwa wa waombolezaji ulijitokeza katika mji wa magharibi mwa Kenya, Kisumu. Watu kadhaa walijeruhiwa wakati wa maombolezo ya Kisumu.
Vilio vya “Baba” na “Sisi ni mayatima” vimesikika miongoni mwa maelfu ya watu waliomiminika mitaani mjini Kisumu, ngome kuu ya uungwaji mkono wa Odinga, wakati jeneza lake lilipowasili kwa helikopta katika uwanja wa jiji hilo.
Raila Odinga, mwenye umri wa miaka 80, alifariki Jumatano nchini India kutokana na kile kinachoshukiwa kuwa mshtuko wa moyo, na kusababisha majonzi makubwa kote nchini, hasa katika eneo la magharibi mwa Kenya ambako kabila lake la Wajaluo linatawala.
Waombolezaji walivunja vizuizi vya usalama na kupanda kuta za uwanja na majengo jirani ili kuweza kuona jeneza. Wasaidizi wa dharura walisema waliwatoa zaidi ya watu 100 walioumia kutoka uwanjani.
“Bila Baba, tumekufa. Hatuna pa kwenda,” alisema Don Pelido, mwenye umri wa miaka 20, aliyekuwa amebanwa dhidi ya kizuizi kimoja.
Wengi walihofia kuwa shughuli ya Jumamosi ingesababisha maafa, ikizingatiwa vurugu zilizotokea kwenye kumbukumbu zilizofanyika Nairobi wiki hii.
Mamia ya waombolezaji wamejeruhiwa Jumamosi katika ibada ya kumbukumbu ya kiongozi wa upinzani wa Kenya, Raila Odinga, wakati umati wa watu uliongezeka, gazeti la The Standard liliripoti kupitia akaunti yake ya X.
Alhamisi, vikosi vya usalama vilifyatua risasi kutawanya umati uliokuwa ukisonga mbele katika uwanja wa Nairobi ambako Odinga alikuwa amewekwa kwa heshima za mwisho, na kuua angalau watu watatu. Ijumaa, katika maombi ya kitaifa yaliyoongozwa na Rais William Ruto katika uwanja mwingine, msongamano wa waombolezaji uliua angalau watu wawili na kujeruhi kadhaa.
“Hatujakubali kuwa ameondoka kweli”
Kwa hakika, Odinga alikuwa kiongozi wa kisiasa mwenye ushawishi mkubwa zaidi wa kizazi chake nchini Kenya. Alihudumu kama Waziri Mkuu kati ya 2008 na 2013, ingawa hakuwahi kufanikiwa kushinda urais licha ya kujaribu mara tano.
Hata hivyo, aliwashinda wapinzani wengi na anasifiwa kama mhusika mkuu katika kurejesha demokrasia ya vyama vingi nchini Kenya miaka ya 1990, na kusimamia katiba ya mwaka 2010 iliyosifiwa sana.
Mwili wa Odinga ulirejeshwa kutoka India Alhamisi. Baada ya heshima za mwisho Kisumu Jumamosi, mwili huo utapelekwa Bondo, karibu na kaunti ya Siaya, nyumbani kwa mababu wa familia, kwa mazishi ya faragha.
Kifo chake kimeacha pengo la uongozi katika upinzani, huku wakosoaji wakimlaumu kwa kushindwa kuandaa mrithi. “Hatujakubali kuwa ameondoka kweli. Bado ni ndoto mbaya,” alisema Maureen Owesi, mmiliki wa duka mjini Kisumu, mwenye umri wa miaka 39.
Makubaliano ya Odinga ya kisiasa na wapinzani wake — akiwemo Rais Ruto mwaka jana — yalimpunguzia uungwaji mkono miongoni mwa vijana, ambao wameandamana kwa wingi miaka miwili iliyopita kupinga utawala mbovu na hali ya uchumi.
Haijulikani kama harakati za Odinga na ushirikiano wake na Ruto vitaendelea baada ya kifo chake, hali inayoiweka Kenya katika njia isiyoeleweka kuelekea uchaguzi wa mwaka 2027 ambao huenda ukawa na mvutano mkubwa.