Kiasi kikubwa cha fedha kinachokusanywa kwa ajili ya ujenzi upya wa Syria kimewashangaza wengi. Baadhi wanatizama kama muujiza wa kipekee. Michango hiyo, ambayo imekuwa ikiendelea tangu katikati ya Agosti mwaka uliopita, huenda ndiyo kampeni ya kuchangisha fedha iliyofanikiwa zaidi duniani. Je, hii ni dalili ya matumaini mapya ya kuijenga upya Syria, au ni mbinu ya baadhi ya watu kujisafisha mbele ya umma?

Mnamo mwaka 2024, wakati wa kampeni za uchaguzi wa urais nchini Marekani, mgombea wa chama cha Democratic, Kamala Harris, alifanikiwa kukusanya zaidi ya dola milioni 47 chini ya saa 24 pekee kutoka kwa wafadhili wake.

Lakini mnamo mwezi Septemba, katika muda sawa, wafadhili huko Idlib, kaskazini mwa Syria, walichangisha takriban dola milioni 208, kiwango kikubwa kisichotarajiwa kwa nchi iliyokumbwa na vita kwa zaidi ya muongo mmoja.

Tangu katikati ya msimu wa kiangazi, kumefanyika takriban kampeni10 katika miji na wilaya mbalimbali nchini humo zenye lengo la kuchangisha fedha kwa ajili ya ujenzi upya wa Syria.

Syria Idlib 2025 | Tukio la kuchangisha fedha kwa ajili ya ujenzi wa jimbo la Idlib
Kampeni ya kuchangisha fedha kwa ajili ya Idlib nchini Syria mnamo Septemba 26, 2025 ambapo zaidi ya dola milioni 208 zilichangishwa.Picha: Bakr Al Kasem/Anadolu Agency/IMAGO

Kampeni tofauti katika miji na wilaya tofauti

Kiasi cha fedha kinachopatikana katika kila kampeni kimeripotiwa na vyombo vya habari vya ndani, ingawa takwimu hizo ni vigumu kuthibitishwa na mashirika huru. Kwa mujibu wa nyaraka ambazo DW imeziona, fedha zote zilizokusanywa zinakaribia dola milioni 500.

Kampeni hizo zimepokelewa kwa shangwe na matumaini makubwa. Kwa Wasyria wengi, ni ishara ya matumaini mapya kwamba nchi yao, iliyoharibiwa vibaya na vita vya wenyewe kwa wenyewe vya muda mrefu, inaweza kufufuliwa tena.

Fadel al-Akl, mwanachama wa kamati ya ukusanyaji fedha tawi la Idlib, amesema kampeni hizo zimejikita katika misingi ya umoja na ushirikiano wa kitaifa.

Soma zaidi kuhusu Syria baada ya al-Assad

Akizungumza na DW, alisema hatua ya kwanza ni kurejesha hali ya kawaida katika vijiji na miji ambako hakuna tena miundombinu, shule, vituo vya afya wala mifumo ya maji. Amesema kampeni hizo zimehusisha watu wa rika na tabaka zote kuanzia matajiri hadi masikini.

Syria Deir ez-Zor 2025 | Kampeni ya kuchangisha fedha kwa ajili ya ujenzi wa jimbo la Deir ez-Zor
Watu wahudhuria kampeni ya kuchanga fedha kwa ujenzi upya wa mkoa wa Deir ez-Zor kaskazini mashariki mwa SyriaPicha: Hisam Hac Omer/Anadolu/picture alliance

Je, wachangiaji wanatoa kwa moyo wa dhati au wanajitakasa?

Wachangiaji wengi wanatoa fedha ndogo kuanzia dola nne, huku mchangiaji mkubwa akiwa ni Ghassan Aboud, bilionea wa Kisyria anayeishi Umoja wa Falme za Kiarabu, ambaye alitoa dola milioni 55 peke yake. Awali, Aboud alionekana kuwa mpinzani wa serikali ya Bashar al-Assad, jambo lililoibua mjadala kuhusu motisha yake ya sasa.

Hata hivyo, si wote wanaoamini nia njema ya michango hiyo. Mwezi Oktoba, mtafiti wa taasisi ya Chatham House ya Uingereza, Haid Haid, aliandika kuhusu jinsi familia tajiri ya Hamsho, inayodaiwa kuwa na uhusiano wa kihalifu na utawala wa zamani wa Assad, ilivyotoa mamilioni ya dola kupitia kampeni mbili tofauti.

Mkaazi mmoja wa Idlib, ambaye hakutaka kutajwa jina, ameiambia DW kwamba baadhi ya wachangiaji wanatoa kwa moyo wa dhati, lakini wapo pia wanaotumia kampeni hizo kama njia ya kujisafisha dhidi ya makosa ya zamani.

Maswali bado yanaibuka kuhusu uwazi wa matumizi ya fedha hizo, nani anazisimamia, na iwapo zitaelekezwa kweli katika ujenzi wa nchi, au zitakuwa chombo cha kisiasa cha kujenga taswira mpya mbele ya umma wa Syria na dunia.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *