
Jeshi la Uganda limekanusha madai ya kuwashikilia wanaharakati wawili wa Kenya Bob Njagi na Nicholas Oyoo, ambao walitekwa nyara mjini Kampala, Uganda, Oktoba 1.
Mawakili wawili wa Uganda walikuwa wamedai kuwa wawili hao walikuwa wanazuiliwa katika kambi ya jeshi huko Mbuya, Kampala.
Katika majibu yao kwa kesi iliyowasilishwa na mawakili wawili kwenye Mahakama Kuu ya Uganda, Jeshi la Uganda (UPDF) lilisema lilifanya uchunguzi na kupekua vituo vyote muhimu katika maeneo yao lakini hakuna taarifa kuhusu wanaharakati hao wawili waliotoweka.
Jeshi hilo lililotajwa kuwa mmoja wa waliohojiwa katika kesi hiyo, limekanusha kuhusika katika utekaji nyara kwa wanaharakati wa Kenya Bob Njagi na Nicholas Oyoo.
Uamuzi wa mahakama kuhusu suala hilo unatarajiwa kutolewa siku ya leo Alhamisi.
Silas Kamanda, Kanali wa UPDF ambaye ni mkurugenzi wa masuala ya kisheria jeshini, aliiambia mahakama kuwa jeshi la Uganda lilifanya uchunguzi na kupekua vituo vyote muhimu vya mahabusu, sajili za watu waliofungiwa, na rekodi za ulinzi, na hawakupata taarifa zozote kuhusu wanaharakati hao Nicholas Oyoo na Bob Njagi.