SPIKA wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mussa Azzan Zungu, ametangaza kuwa kesho, Novemba 13, 2025, Bunge litakuwa na kikao maalum cha kuthibitisha uteuzi wa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na uapisho wa Naibu Spika wa Bunge.
Taarifa hiyo imetolewa leo jijini Dodoma na Spika Zungu alipokuwa akiahirisha Kikao cha Pili cha Mkutano wa Kwanza wa Bunge jipya, ambapo alisisitiza umuhimu wa wabunge wote kuhudhuria kikao hicho kutokana na uzito wa ajenda zilizopangwa. “Nawaomba wabunge wote wahudhurie kikao cha kesho bila kukosa, kwa kuwa shughuli zitakazofanyika ni za msingi katika kuanzisha rasmi Serikali mpya,” alisema Spika Zungu.
Kikao hicho maalum kinatarajiwa kufanyika baada ya Bunge kukamilisha kiapo cha uaminifu na ahadi ya uzalendo kwa wabunge wateule hatua iliyoashiria ukamilishaji wa taratibu za awali za Bunge jipya (2025–2030).Kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 (kama ilivyorekebishwa), uteuzi wa Waziri Mkuu hufanyika kwa kufuata utaratibu maalumu unaoanza mara baada ya Rais kuapishwa rasmi kushika madaraka. .SOMA: Huyu ndiye Mussa Zungu
Ibara ya 51(1) ya Katiba inaeleza kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania anateua Waziri Mkuu kutoka miongoni mwa wabunge wa kuchaguliwa, na uteuzi huo lazima uthibitishwe na Bunge kwa azimio la wabunge wengi. Aidha, Ibara ya 51(2) inaelekeza kuwa uteuzi huo ufanyike ndani ya siku kumi na nne (14) tangu Rais kuapishwa.
Baada ya kuthibitishwa na Bunge, Waziri Mkuu huapishwa kwa kiapo cha uaminifu, uadilifu na ahadi ya kulitumikia taifa mbele ya Rais au mwakilishi aliyeidhinishwa naye, kabla ya kuanza rasmi kutekeleza majukumu yake. Kwa mujibu wa Ibara ya 52(1) ya Katiba, Waziri Mkuu ndiye kiongozi wa shughuli za Serikali bungeni na ndiye anayesimamia utekelezaji wa sera na shughuli zote za Serikali ya Muungano kwa niaba ya Rais.
Utaratibu huu wa kikatiba unaimarisha misingi ya uwajibikaji, ushirikiano na uwazi kati ya Serikali na Bunge huku ukihakikisha kuwa uteuzi wa Waziri Mkuu hauishii katika mamlaka ya Rais pekee, bali pia unapata ridhaa ya wawakilishi wa wananchi. Spika Zungu amehitimisha kwa kuwataka wabunge na wananchi kwa ujumla kufuatilia kwa karibu kikao cha kesho, akisema ni hatua muhimu katika kujenga Serikali yenye uwajibikaji na inayoongozwa kwa misingi ya Katiba.
