
Zaidi ya watu 16,000 wameuawa tangu mwaka 2022 huko Haiti, kisiwa kilichokumbwa na ghasia za magenge, Umoja wa Mataifa umesema katika ripoti yake. Aidha Umoja wa Mataifa umeonya ukisema kwamba bila msaada wa kimataifa, “hali mbaya zaidi inaweza kutokea.”
Onyo hili linakuja siku moja wa baada ya Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, kupitisha azimio la kuongeza walinda usalama nchini Haiti kuungana na wale kutoka Kenya, kukabiliana na makundi hayo yenye silaha.
“Idadi ya watu walio hatarini inatisha: nusu ya watu, watu milioni sita, ikiwa ni pamoja na watoto milioni 3.3, wanahitaji msaada wa kibinadamu,” Kamishna Mkuu wa Umoja wa Mataifa wa Haki za Kibinadamu Volker Türk ameliambia Baraza la Haki za Kibinadamu huko Geneva.
Haiti, taifa maskini zaidi katika bara la Amerika, limekumbwa na vurugu za magenge yanayoshutumiwa kwa mauaji, ubakaji, na utekaji nyara. Kutokana na hali ya ukosefu wa utulivu wa kisiasa, idadi iliyorekodiwa ya karibu watu milioni 1.3 wamekimbia makazi yao kutokana na shughuli za magenge, Umoja wa Mataifa ulionya mwezi Juni.
Kulingana na Umoja wa Mataifa, zaidi ya watu 3,000 walifariki katika ghasia nchini Haiti katika nusu ya kwanza ya mwaka 2025. Katika kujaribu kuzuia unyanyasaji wa magenge yanayodhibiti karibu mji mkuu wote, Port-au-Prince, Baraza liliidhinisha mnamo mwaka 2023 kuundwa kwa Misheni ya Kimataifa ya Usalama (MMAS), inayoongozwa na Kenya, kusaidia polisi wa Haiti walioshindwa kukabilina na magenge hayo. Hata hivyo, kutokuwa na vifaa vya kutosha, ufadhili wa chini, na maafisa elfu moja tu kati ya 2,500 wanaotarajiwa, matokeo yake yamekuwa mabaya zaidi.