
Dar es Salaam. Msanii wa Bongo Movies, Zaiylissa amezungumzia maisha yake baada ya kuachana na aliyekuwa mume wake Haji Manara, akisema hajatingishika na kwamba sasa mambo ndio yanazidi kumnyookea.
Zaiylissa ambaye anatamba kwenye tamthilia ya Jua Kali, amesema kuachika kwake kwenye ndoa hakujamfanya akate tamaa ya kuendelea na maisha mengine ya kawaida.
Kwenye mahojiano aliyofanya na Mwananchi, Zaiylissa amesema kuna wanawake wengine wakiachwa huwa wanakuwa kama wamepatwa na ugonjwa wa kuwafanya washindwe kufanya chochote maishani wakiwaza tu mapenzi, jambo ambalo halipaswi kufanywa na mwanamke anayejitambua.
“Ukweli ni kwamba kuachika kwangu hakujanifanya nishindwe kuendelea na maisha yangu ya kujitafutia riziki. Kwanza nilipoachwa ndiyo maisha yakaninyookea na hivi ninavyokwambia tayari niko katika uhusiano mpya mzuri wenye upendo hivyo yaliyopita nishayasahau,” amesema muigizaji huyo.
Zaiylissa alifunga ndoa na Haji Manara Januari 24, 2024 iliyodumu kwa miezi 14 ambapo kwa mujibu wa waliyoyaweka wenyewe mitandaoni ilivunjika Aprili 9, 2025
Hii ilikuwa ni ndoa ya pili kwa Zaiylissa, ambapo ya kwanza alifunga mwaka 2023 na msanii wa singeli, Dullah Makabila ambayo ilidumu kwa mwezi mmoja tu.