
Waandishi wa habari huhatarisha maisha yao kila siku ili kuufikisha ukweli kwa umma, lakini mashambulizi mengi dhidi yao hubaki bila kuadhibiwa.
Katika maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Kukomesha Kutoadhibiwa kwa Uhalifu Dhidi ya Waandishi wa Habari, inayoadhimishwa kila tarehe 2 Novemba, Umoja wa Mataifa unataka haki kwa wale waliowanyamazishwa na unatoa wito wa kulindwa kwa wale wanaoendelea kufichua matumizi mabaya ya madaraka iwe katika maeneo ya vita au kwenye majukwaa ya kidijitali ambako ukatili huenea kwa kasi.
“Katika jitihada zao za kutafuta ukweli, wataalamu wa habari duniani kote wanakabiliwa na hatari zinazoongezeka, ikiwemo matusi, vitisho vya kisheria, mashambulizi ya kimwili, kufungwa na kuteswa.
Baadhi yao hata huuawa,” alisema Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa.
Kutoadhibiwa
Katika ujumbe wake kwa siku hii, António Guterres alikumbusha kuwa karibu mauaji tisa kati ya kumi ya waandishi wa habari duniani kote hayajawahi kutatuliwa.
Amesema Gaza imekuwa “mahali hatari zaidi kwa waandishi wa habari katika mzozo wowote,” na akatoa wito wa kufanyika kwa uchunguzi huru na usio na upendeleo kuhusu uhalifu wote wa aina hiyo.
Guterres alionya kuwa kutoadhibiwa “si tu ukosefu wa haki kwa waathirika na familia zao, bali pia ni shambulio kwa uhuru wa vyombo vya habari, ni mwaliko wa kuendeleza ukatili zaidi na ni tishio kwa demokrasia yenyewe.”
Ili kukomesha janga hili, alihimiza serikali “kuchunguza kila kesi, kuwafikisha wahalifu wote mahakamani, na kuhakikisha kuwa waandishi wa habari wanaweza kufanya kazi zao kwa uhuru kila mahali.”
Mashambulizi ya mtandaoni dhidi ya wanawake
Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO), ambalo linaongoza juhudi za kimataifa za kulinda uhuru wa vyombo vya habari, linaongoza kampeni ya mwaka huu inayolenga ongezeko la matumizi ya teknolojia za kidijitali kushambulia waandishi wa habari wanawake.
Kupitia mpango wa “GBV Chat”, unaolenga kuongeza uelewa kuhusu ukatili wa kijinsia unaochochewa na akili bandia (AI) dhidi ya waandishi wa habari wanawake, UNESCO inaonya kuwa kuongezeka kwa teknolojia hii ya kizazi kipya kumeongeza ukubwa na athari za unyanyasaji wa mtandaoni.
“Wakati maudhui ya uongo, au deepfake, ya mwandishi wa habari yaliyotengenezwa kwa akili bandia yanaposambaa mtandaoni, siyo tu kwamba yanashambulia taswira yake, bali pia uaminifu wake, usalama wake na sauti yake,” lilisema shirika hilo la Umoja wa Mataifa.
Mashambulizi haya ni sehemu ya ukatili wa kijinsia unaochochewa na teknolojia, aina mpya ya unyanyasaji inayolenga kunyamazisha, kudhalilisha na kupunguza heshima ya wanawake kwenye vyombo vya habari.
Vitisho na mashambulizi
Utafiti wa UNESCO umeonesha kuwa asilimia 73 ya waandishi wa habari wanawake wamekumbwa na vitisho vya mtandaoni, na mmoja kati ya wanne ameshambuliwa ana kwa ana kutokana na hayo.
Kwa ujumla, asilimia 58 ya wanawake na wasichana vijana duniani wamewahi kunyanyaswa kwenye mitandao ya kijamii, jambo linaloonyesha ukubwa wa tatizo hili.
“Majukwaa ya kidijitali lazima yawe salama kwa wale wanaokusanya na kusambaza habari,” alisema Katibu Mkuu. “Wakati waandishi wa habari wananyamazishwa, sisi sote tunapoteza sauti zetu.”
Ujumbe kutoka Umoja wa Mataifa na waandishi wa habari wanaotekeleza majukumu yao ni wazi: Haki kwa waathirika wa uhalifu unaofanywa kwa sababu tu ya kutekeleza wajibu wao lazima iwe jambo lisilojadiliwa, na maeneo ya kidijitali lazima yarudishwe mikononi mwa wale wanaotumia teknolojia kwa manufaa ya amani badala ya kueneza hofu na chuki.