
Chanzo kimoja cha serikali kimeliambia shirika la habari la AFP, ikiwa ni wiki moja tu baada ya wanamgambo wa RSF kuuvamia mji muhimu wa El-Fasher. RSF ambao wamekuwa vitani na jeshi tangu Aprili 2023, wanaonekana kuandaa shambulio katika eneo la kati la Kordofan baada ya kuteka El-Fasher, ngome ya mwisho ya jeshi huko Darfur, zaidi ya wiki moja iliyopita. Kundi linaloitwa Quad — linalojumuisha Marekani, Misri, Umoja wa Falme za Kiarabu na Saudi Arabia — kwa miezi kadhaa limekuwa likiendesha juhudi ya diplomasia inayolenga kupata makubaliano ya kusitisha mapigano katika mgogoro wa zaidi ya miezi 30 nchini Sudan.
Mnamo Septemba, mataifa hayo manne yenye nguvu yalipendekeza makubaliano ya kuweka chini silaha kwa miezi mitatu kwa sababu za kibinaadamu, ikifuatiwa na makubaliano ya kudumu ya kusitisha mapigano na utawala wa mpito wa miezi tisa kupisha serikali ya kiraia, yakidokeza kuwatenga jeshi na RSF kutoka katika mchakato wa mpito.
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ametoa wito wa kusitishwa machafuko na kuonya kuwa mzozo wa Sudan unazidi kuwa mbaya zaidi.