
Chuo Kikuu cha Sheffield Hallam, kaskazini mwa Uingereza, kinakabiliwa na kashfa ya kidiplomasia na China. Uchunguzi uliofanywa na BBC na Gazeti la The Guardian unaonyesha kwamba, chini ya shinikizo kutoka Beijing, chuo kikuu kimesitisha utafiti wa Laura Murphy, mtaalamu wa utumwa wa kisasa, lakini zaidi ya yote, maarufu kimataifa kwa utafiti wake kuhusu kazi ya kulazimishwa ya Wauyghur nchini China. Beijing inaona utafiti huu kuwa propaganda dhidi ya China.
Imechapishwa:
Dakika 3 Wakati wa kusoma
Matangazo ya kibiashara
Nyaraka zilizochapishwa na vyombo viwili vya habari vya Uingereza zinaonyesha kwamba Chuo Kikuu cha Sheffield Hallam kimekuwa kikikabiliwa na shinikizo la China kwa miaka miwili iliyopita. Shinikizo hili lilianza mwaka wa 2021 kwa kuchapishwa kwa ripoti ya Profesa Laura Murphy. Ripoti hiyo ililenga kazi ya kulazimishwa ya Wauyghur katika tasnia ya paneli za jua. Laura Murphy alisifiwa na chuo kikuu chake kwa ripoti hii. Ubalozi wa China jijini London uliishutumu kama ripoti ya uwongo na isiyokamilika.
Tangu wakati huo, shinikizo limeongezeka. Kulingana na uchunguzi wa Gazeti la The Guardian na BBC, hati ya ndani ya chuo kikuu inarejelea taarifa kutoka Wizara ya Mambo ya Nje ya China inayolaani matamshi dhidi ya China ya Sheffield Hallam. Beijing ilifunga tovuti ya chuo kikuu nchini China. Wafanyakazi wa chuo kikuu kilichopo China pia walitishwa na kuhojiwa kwa saa nyingi.
Kutokana na shinikizo hili, mwezi Februari imwaka huu, Laura Murphy aligundua kwamba hangeweza tena kuendelea na utafiti wake kuhusu kazi ya kulazimishwa huko Xinjiang. Baada ya kusalimu amri, hatimaye alirejeshwa kazini na akaomba msamaha kutoka chuo kikuu.
“Inatisha, lakini haishangazi”
Kwa mtafiti mkuu wa Ujerumani Adrian Zenz, mkurugenzi wa masomo ya Kichina katika taasisi ya Foundation for the Memory of Victims of Communism, jambo hili linatisha, lakini halishangazi.
“Inatisha kwa sababu ya asili ya wazi ya vitisho vinavyotolewa na idara za usalama za China dhidi ya taasisi ya kitaaluma ya Magharibi.” “Pia inatisha kwa sababu wanafanikiwa kuzuia uhuru wa vyuo vikuu vya Magharibi kwa urahisi,” anasema. “Lakini wakati huo huo, haishangazi, kwa sababu tumejua kwa miaka kadhaa kwamba vyuo vikuu vya Magharibi viko katika hatari ya aina hii ya shinikizo. Vinategemea kwa kiasi kikubwa wanafunzi wa China, au wanaamini kutegemewa,” mtafiti anaeleza.
Vtendo vya kawaida vya vitisho
Ingawa aina hii ya kesi haishangazi, bado ni nadra sana kuwa na taarifa nyingi kuhusu jinsi China inavyoshinikiza. Ni bahati kwamba kesi ya Laura Murphy ni ya umma, lakini vyuo vikuu vingi huficha aina hizi za kesi au hukataa na kusema sio suala la shinikizo hata kidogo, anaelezea Vanessa Frangville, profesa wa masomo ya Kichina na mkurugenzi wa EAST, kituo cha utafiti cha Asia Mashariki katika Chuo Kikuu Huria cha Brussels.
“Ikiwa tutachukua Sciences Po Paris, kwa mfano, ambayo miaka michache iliyopita ilikataa kuandaa mkutano wa Dalai Lama na kusema, ‘Hapana, hapana, hii haina uhusiano wowote na shinikizo la China,’ ni dhahiri kwamba ilikuwa shinikizo la China. Kwa sababu kuna makubaliano mengi kati ya Sciences Po na China. Hakuna chuo kikuu kitakachokubali kushinikizwa na kusalimu amri, lakini Sheffield haina chaguo.” Hakuna chaguo, kwa sababu Laura Murphy kwanza alitaka kukishtaki chuo kikuu, na hivyo akapata hati ambazo hangeweza kuzipata vinginevyo.
Shinikizo zinazohatarisha utafiti
Kulingana na Adrian Zenz, mwenyewe mwathiriwa wa kampeni ya vitisho kwa kazi yake kuhusu Uyghur, shinikizo hilo liliongezeka wakati wa nusu ya pili ya muhula wa Xi Jinping, kati ya mwaka 2017 na 2018. Utafiti pia ulifanywa kuwa mgumu zaidi baada ya mlipuko wa UVIKO-19 na kufungwa kwa baadhi ya maeneo kwa watafiti.
“Hili haliathiri mtafiti mmoja tu, haliathiri taasisi moja tu, hali ya aina hii inaathiri jamii nzima ya kisayansi ya kimataifa. Ni kubwa sana katika suala la uhuru wa kitaaluma. Ina athari kwa maarifa yetu wenyewe na taarifa tunazoweza kutoa kwa watunga sera,” anahofia Vanessa Frangville wa Chuo Kikuu Huria cha Brussels. Kwake, aina hii ya hali inaweza kusababisha watafiti kuzingatia mada pekee ambapo kuna makubaliano ya jumla.
Kwa sababu hizi zote, Vanessa Frangville anatumai kwamba kesi ya Laura Murphy itakuwa mfano, na kwamba vyuo vikuu vingine vitalaani shinikizo la China. Shinikizo hili ni jambo ambalo mtafiti Adrien Zenz analiunganisha na jambo pana la “ukandamizaji wa kimataifa.”