
Guinea inaadhimisha kumbukumbiya ya mwaka mmoja tangu kutokea tukio baya la watu kukanyagana lililosababisha vifo vingi katika uwanja wa soka wa Nzérékoré.
Imechapishwa:
Dakika 2 Wakati wa kusoma
Matangazo ya kibiashara
Mwaka mmoja uliopita leo, Desemba 1, watu kadhaa walipoteza maisha wakati wa mechi ya mpira wa miguu huko Nzérékoré. Wakati wa fainali ya mashindano yaliyofanyika kwa heshima ya Jenerali Mamadi Doumbouya, uwanja uliojaa watu wengi katika mji mkuu wa Mkoa wa Misitu ulishuhudia tukio baya lililosababisha vifo vingi. Idadi rasmi ya vifo iliyotolewa na serikali ya Guinea inafikia 56, lakini mashirika yasiyo ya kiserikali katika eneo hilo yanakadiria kuwa zaidi ya watu 140 walipoteza maisha. Licha ya malalamiko yaliyowasilishwa na familia za waathiriwa, mwaka mmoja baadaye, vyombo vya sheria vyaGuinea wala serikali haijatoa taarifa mpya kuhusu uchunguzi.
Wakati mashindano kadhaa ya mpira wa miguu kote Guinea yakiandaliwa na makundi yanayomuunga mkono Jenerali Mamadi Doumbouya na kwa usaidizi wa serikali, yale ya Nzérékoré, kusini mashariki mwa nchi, yalitakiwa kuwa makubwa. Kampeni kubwa ya utangazaji, usafiri bila malipo kwa mashabiki, na kualikwa kwa wageni wa heshima yote haya yalikuwa sehemu ya mpango huo.
Siku hiyo, maelfu ya watazamaji walikusanyika kwenye uwanja wa Aprili 3 huko Zaly, ukumbi mdogo sana na uliokuwa ukijengwa kwa muongo mmoja. Baada ya uamuzi wa marefa uliopingwa na kuingiliwa kwa wanasiasa, mawe yalirushwa uwanjani. Polisi walirusha gesi ya machozi.
Hofu ilifuata. Mkanyagano wa kutisha ulizuka ndani ya uwanja, ambao ulikuwa na njia moja tu ya kutokea. Serikali ilitangaza vifo 56. Idadi hii ya muda haikurekebishwa kamwe, huku ripoti ya uchunguzi ya mashirika yasiyo ya kiserikali katika Mkoa wa Misitu ikihesabu zaidi ya mara mbili ya idadi hiyo, watu 140 walipoteza maisha, hasa watoto.
Ripoti hiyo inaangazia hasa nia ya serikali ya kuficha ukweli, huku mashahidi wengi wakidai kuwa waliona vikosi vya usalama vikisafirisha miili hadi kambi yao ya kijeshi. Hii ni miili ambayo familia bado zinaitafuta leo.
Familia kadhaa zimewasilisha malalamiko dhidi ya waandaaji, pamoja na Mawaziri wa Michezo na Mifugo, haswa kwa “mauaji, mauaji ya bila kukusudia, kuhatarisha maisha ya wengine, na kuficha maiti.” Lakini mwaka mmoja baadaye, vyombo vya sheria vya Guinea wala serikali haijatoa taarifa mpya kuhusu uchunguzi huo, ingawa mashahidi wengi wanasema waliona vikosi vya usalama vikisafirisha miili hadi kambi ya kijeshi ya jiji hilo. Emmanuel Fassou Sagno, kiongozi wa muungano wa mashirika yasiyo ya kiserikali huko Nzérékoré, anaelezea dhiki ya familia hizo.
Kulingana na wakili wao, Paul Lazard Gbilimou, malalamiko yao hayajaenda popote, licha ya pande za kiraia kusikilizwa na jaji anayechunguza. Leo huko Nzérékoré, familia hizo zimepanga sherehe ya kuwakumbuka waathiriwa.