Droni za Urusi zaigeuza Kherson kuwa “safari ya binadamu”Droni za Urusi zaigeuza Kherson kuwa “safari ya binadamu”

Wakaazi wa Kherson kusini mwa Ukraine wanaendelea kuishi katika hofu kutokana na wimbi la mashambulizi ya kila mara ya droni za Urusi, ambayo hata baada ya ukombozi wa mji mwaka 2022 yamekuwa yakiwalenga raia bila kusita.

Kwa mujibu wa ripoti ya Umoja wa Mataifa, droni hizo zimekuwa zikipiga maeneo ya makaazi kwa makusudi, hali iliyosababisha vifo na majeraha kwa mamia ya watu na kuacha athari kubwa ya kiakili na kimwili kwa jamii.

Droni hizo hutumia kamera kutambua na kufuatilia malengo, hasa magari yanayoonekana barabarani, bila kujali kama ni ya abiria, mizigo au hata magari ya wagonjwa, jambo linalofafanua ukubwa wa ukiukaji wa sheria za kijeshi.

Ripoti moja iliyopatikana na Shirika la Habari la AP kutoka kwa kikosi maalumu cha kufuatilia matumizi ya zana za kielektroniki inaonyesha droni hupaa kwa wingi kwenye maeneo yenye magari, zikifanya mashambulizi ya ghafla na yasiyotabirika.

Dmytro Liashok, kamanda wa kikosi cha 310 kinacholinda anga ya kilomita 470 kusini mwa Ukraine, amesema angalau droni 300 huruka kuelekea Kherson kila siku, na zaidi ya droni 9,000 ziliripotiwa mwezi Oktoba pekee.

Ujerumani Berlin 2025 | Filamu ya makala Kherson: Human Safari | Mlipuko wa maandamano kwa bendera ya Ukraine wakati wa uvamizi
Mwanaume anakimbia akiwa amebeba bendera ya Ukraine wakati wa maandamano; siku za kwanza za uvamizi huko Kherson. Taswira kutoka filamu ya makala “Kherson: Human Safari,” inayochora maisha ya watu katika mji wa Kherson unaoshambuliwa kwa mabomu.Picha: Oleskandr Kornyakov

Idadi ya droni yazidi kuongezeka huku mashambulizi yakigeuka ya kimakusudi dhidi ya raia

Kwa mujibu wa Liashok, asilimia 93 ya droni za Urusi hazifiki shabaha zao za kijeshi, badala yake zikimalizia kuangukia maeneo yenye raia, hali inayoongeza vifo na uharibifu wa mali kwa kiwango kikubwa.

Mbali na droni,jeshi la Urusi limekuwa likitumia mizinga na mabomu ambayo yameongeza ukali wa mashambulizi katika mji huo, ingawa kikosi cha ulinzi wa Ukraine kimefanikiwa kuharibu zaidi ya asilimia 90 ya zana hizo.

Ripoti ya ofisi ya haki za binadamu ya Umoja wa Mataifa inaonyesha kuwa mashambulizi ya droni ndogo za masafa mafupi ndiyo yanayoongoza kwa kuua na kujeruhi raia katika maeneo ya kusini mwa Ukraine.

Tangu Julai 2024, zaidi ya raia 200 wameuawa na zaidi ya 2,000 kujeruhiwa katika maeneo yanayolengwa mara kwa mara, idadi kubwa yao ikiwa wanaume waliokuwa wakijaribu kufanikisha shughuli zao za kila siku.

Zaidi ya makaazi 3,000 yameharibiwa au kubomolewa, na mji wa Kherson umegeuka eneo la vifo vya mara kwa mara, huku vita vikilenga zaidi watu wasiokuwa na uwezo wa kujilinda.

Baadhi ya Waukraine waamua kutoroka kuliko kupigana na Urusi

To view this video please enable JavaScript, and consider upgrading to a web browser that supports HTML5 video

Umoja wa Mataifa wataja mashambulizi kama uhalifu dhidi ya binadamu

Mjumbe wa Umoja wa Mataifa Angelina Jolie, aliyefanya ziara ya kushtukiza Kherson, alisema walipata taharuki walipoona droni ikipaa juu yao, akibainisha kuwa hali hiyo ndiyo maisha ya kila siku kwa wakaazi.

Katika hospitali ya Kherson, majeruhi wengi wanaendelea kutibiwa kutokana na milipuko ya droni, akiwemo mwanamke mzee mwenye umri wa miaka 70, Nataliia Naumova, ambaye alijeruhiwa mguuni baada ya droni kulipuka karibu naye.

Naumova amesema mashambulizi hayo yameharibu nyumba nyingi, huku madirisha yakivunjika na kuta kuharibika, na wakaazi kulazimika kuziba mianya kwa mabodi ili kuendelea kuishi katika hali ya hatari.

Wakaazi wengi wanasema kuwa mji unaonekana kama eneo la majaribio ya kijeshi, ambapo maisha yao yanadharauliwa, na droni zinawafuata kama “wanyama kwenye safari” wanapojaribu kutafuta chakula au kuelekea hospitali.

Umoja wa Mataifa umeelezea mashambulizi haya kama uhalifu dhidi ya binadamu, na umetoa wito kwa Urusi kusitisha mara moja mashambulizi yanayolenga raia na kuheshimu sheria za kimataifa za vita.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *