Urusi imetangaza kuwa mazungumzo ya saa tano kati ya Rais Vladimir Putin na wajumbe wa Rais Donald Trump katika ikulu ya Kremlin hayakuzaa makubaliano kuhusu mpango wa amani wa kumaliza vita vya Ukraine, ikiwa ni ishara kuwa safari ya kidiplomasia bado ni ndefu.

Trump, ambaye mara kwa mara ameeleza kukerwa na kushindwa kwa Marekani kumaliza mgogoro huo wa Ulaya, alituma mjumbe wake maalumu Steve Witkoff na mkwewe Jared Kushner kuongoza mazungumzo hayo yaliyodumu hadi usiku wa manane.

Mshauri wa ngazi ya juu wa Kremlin kuhusu masuala ya nje, Yuri Ushakov, alisema baadhi ya mapendekezo ya Marekani hayakukubalika kwa Moscow, huku akiongeza kuwa bado kuna kazi kubwa mbele ya pande zote.

Baada ya mazungumzo, Witkoff alielekea ubalozi wa Marekani mjini Moscow kutoa taarifa mpya kwa Ikulu ya White House, ilhali Kremlin ikisisitiza kuwa hakuna mkutano wa moja kwa moja uliopangwa kati ya Putin na Trump kwa sasa.

Ushakov hata hivyo alieleza kuwa mazungumzo yalikuwa “ya kujenga” na akasisitiza kuwa fursa za ushirikiano wa kiuchumi kati ya Marekani na Urusi bado ni kubwa licha ya mvutano wa kisiasa.

Urusi Moscow 2025 | Vladimir Putin akutana na Steve Witkoff Kremlin
Rais wa Urusi Vladimir Putin na mshauri wa sera za nje Yuri Ushakov wakihudhuria mkutano na mjumbe maalumu wa Rais wa Marekani Donald Trump, Steve Witkoff, pamoja na mkwewe Jared Kushner katika Kremlin, Moscow, Urusi, Desemba 2, 2025.Picha: Kristina Kormilitsyna/Sputnik/Pool via REUTERS

Tofauti za kimsimamo zinaendelea kutawala suala la Ukraine

Ushakov alitangaza pia kuwa Putin alituma ujumbe na salamu kwa Trump kupitia wajumbe hao, lakini maelezo ya kina ya mazungumzo hayakufichuliwa hadharani kwa kile alichokiita “kuheshimu mwendelezo wa mazungumzo.”

Mazungumzo hayo yaliangazia “tatizo la mipaka,” neno ambalo Kremlin hutumia kurejea madai yake ya kudai eneo lote la Donbas, ingawa Ukraine bado inadhibiti zaidi ya kilomita za mraba 5,000 za ardhi inayodaiwa na Urusi.

Ushakov aliongeza kuwa baadhi ya mapendekezo ya Marekani yalionekana kukubalika, lakini mengine “hayafai kabisa” kwa maslahi ya Urusi, na kusisitiza kuwa kazi ya majadiliano itaendelea.

Witkoff na Kushner waliingia Kremlin kupitia Red Square kwa matembezi yaliyopita kaburi la Lenin, wakikutana na Putin, Ushakov na mjumbe maalumu Kirill Dmitriev kwa mazungumzo yaliyotafsiriwa.

Trump, akizungumza kutoka Washington, alieleza kuwa vita nchini Ukraine vimeendelea kuwa “mchanganyiko mgumu,” akitaja takwimu za zaidi ya watu 25,000–30,000 wanaouawa au kujeruhiwa kila mwezi.

Urusi Moscow 2025 | Mkutano wa wajumbe wa Marekani Witkoff na Kushner na Putin Kremlin
Mjumbe wa rais wa Urusi Kirill Dmitriev, mjumbe maalumu wa Rais wa Marekani Donald Trump Steve Witkoff, na mkwewe Jared Kushner katika mkutano na Rais wa Urusi Vladimir Putin katika Kremlin, Moscow, Urusi, Desemba 2, 2025.Picha: Alexander Kazakov/Sputnik/Pool/REUTERS

Ulaya na Ukraine zatia shaka mazungumzo ya Marekani na Urusi

Vita hivyo vilivyoanza Februari 2022 vimezusha mvutano mkubwa zaidi kati ya Moscow na mataifa ya Magharibi tangu Vita Baridi, na juhudi zozote za makubaliano ya amani zinapokelewa kwa umakini mkubwa barani Ulaya.

Nyaraka zilivuja Novemba zikionyesha rasimu ya mapendekezo 28 ya amani ya Marekani, na kusababisha taharuki mjini Kyiv na miongoni mwa mataifa ya Ulaya waliodai rasimu hiyo ilipendelea madai makuu ya Moscow.

Hatimaye mataifa ya Ulaya yaliwasilisha pendekezo mbadala, na Marekani pamoja na Ukraine zikaeleza mjini Geneva kuwa zimeunda “mfumo ulioboreshwa wa amani,” ingawa maelezo ya ndani hayakutolewa hadharani.

Rais Volodymyr Zelenskiy, akizungumza mjini Dublin, alisema matokeo ya mazungumzo ya Moscow yana uzito mkubwa lakini akaonya kuwa Marekani huenda ikapoteza hamasa katika mchakato wa amani iwapo mazungumzo yatachukua muda mrefu.

Zelenskiy aliongeza kuwa mjumbe wa Ukraine Rustem Umerov anatarajiwa kukutana na washauri wa usalama wa Ulaya mjini Brussels na baadaye kuelekea Washington kuendelea na uratibu wa mazungumzo ya amani, akisisitiza kuwa Ukraine haitakubali makubaliano yoyote “yatakayofanyika nyuma ya mgongo wa nchi yake.”

Chanzo: rtre

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *