Majira ya saba mchana,kwa saa za Kinshasa, mbele ya mabunge yote mawili yaliyokutana kwa pamoja, Félix Tshisekedi alitoa hotuba yake ya kila mwaka kuhusu hali ya taifa. Hotuba iliyoelezwa kuwa ya muhimu sana, hasa wakati ambapo mapigano mashariki yamechachamaa tena, na waasi wanasogea kwa kasi kuelekea Uvira.
Katika hotuba yake, kiongozi huyo wa nchi alimshtumu kwa mara nyingine tena jirani yake rais wa Rwanda Paul Kagame kwa kuyaunga mkono makundi ya M23 na kwa kuyavuruga makubaliano ya Washington, makubaliano yaliyosainiwa siku chache tu zilizopita.
“Licha ya nia njema tuliyoonyesha kwenye makubaliano yaliyopitishwa hivi karibuni, ni wazi kwamba Rwanda imeanza kuvunja ahadi zake. Siku moja tu baada ya kusainiwa, majeshi ya ulinzi ya Rwanda yaliunga mkono mashambulizi ya silaha nzito yaliyotokea kutoka Bugarama, na kusababisha uharibifu mkubwa wa maisha na mali huko Kaziba, Katogota na Lubarika.”
Kuhusu mazungumzo yanayoendelea nchini Qatar, amesema kwamba lengo lake kuu ni kuhakikisha kujiondoa kwa wapiganaji wa AFC/M23. Na kwa mujibu wake, makubaliano ya Washington yanathibitisha kuondoka kwa majeshi ya Rwanda nchini DRC.
Lakini wakati anazungumza huko Kinshasa, hali inabadilika ghafla kwenye uwanja wa mapigano. Mji wa Sange, takriban kilomita 30 kutoka Uvira, umeangukia mikononi mwa AFC/M23.
Makundi ya waasi yazidi kuimarika Mashariki mwa Kongo
Video iliyosambaa sana kwenye mitandao ya kijamii inaonyesha waasi wakiingia kwa misururu ya magari wakitokea Bwegera na Luberizi walikokuwa wameteka usiku uliopita. Huu ni ushindi wa kasi unaoongeza hofu kwa wakazi wa Kivu Kusini
Katika hotuba yake, Tshisekedi alisisitiza pia “mafanikio yake chanya” na mipango yake ya ujenzi wa kiuchumi na kijamii. Lakini ujumbe huu haujawashawishi wakazi wa mashariki. Huko Goma, wakazi wanasema hotuba hii haina uhusiano na maisha yao ya kila siku. Philemon Ruzinge, mtetezi wa haki za binadamu anayeishi Goma.
“Kabla hata hajatoa hotuba mbele ya Bunge, tayari tulikuwa tumepoteza Luvungi. Hilo halitupi tena moyo wa kumsikiliza. Anarudia maneno yale yale. Jana Kagame alikuwa mshirika, wakasaini makubaliano; leo anamuita adui. Hotuba yake inawahusu tu wabunge walioko mbele yake, maana hao wabunge hawatufanyii chochote sisi.”
Kati ya kusonga kwa waasi, mashambulizi ya silaha nzito, na kushindikana mara kwa mara kwa hatua ya kusitisha mapigano, hali ya kutoaminiana inaendelea kutawala katika maeneo ambayo Tshisekedi mwenyewe aliita “maeneo mekundu.”
Kwa wakazi wengi wa Mashariki, hotuba hii mpya ya mkuu wa nchi inaonekana kama marudio ya yale ya zamani , si mwanzo mpya. Katika mji wa Uvira, wimbi la wakimbizi wa vita limesababisha hali mbaya ya kibinadamu, huku msaada wa kibinadamu ukitarajiwa kuchelewa kufika katika eneo hilo.
