Kongo yasema M23 bado wako Uvira licha ya kudai kujiondoaKongo yasema M23 bado wako Uvira licha ya kudai kujiondoa

Licha ya tangazo hilo, waasi wa M23, bado wako Uvira, mashariki mwa Kongo, na mapigano yanaendelea katika maeneo ya karibu.

Kulingana na vyanzo rasmi,licha ya tangazo la kundi la waasi wa M23, wapiganaji wenye silaha bado wanaonekana katika mji huo. Waziri wa Habari na Msemaji wa Serikali, Patrick Muyaya amewashutumu waasi hao kwa kuendeleza vita, siku chache tu baada ya kusaini makubaliano ya amani na kulitaja tangazo lao la kuondoka kama upotoshaji. ”Huu ni upotoshaji, kwa sababu, kama unavyojua, umewahi kusikia M23, ambao kimsingi ni mtoto wa Rwanda, wakikana kuhusika katika mchakato wa Washington. Inakuwaje shinikizo limewekwa wazi kwa Rwanda, sasa M23 ndio inajitokeza na kuteseka wakisema, “Sikiliza mimi ndiye mwenye makosa, naondoka Uvira”? Ni dhahiri huu ni ujanja wa kumvuruga mpatanishi ambaye ni Marekani, aliyejitolea kuchukua hatua, kwa sababu ni wazi kuwa kilichotokea Uvira hakikubaliki.”

Warundi walikwama mpakani kutokana na machafuko katika eneo la Uvira
Raia wa Burundi walikwama kwenye kivuko cha mpakani cha Kavimvira kati ya Kongo na Burundi wakijaribu kuvuka kuingia BurundiPicha: Jospin Mwisha/AFP/Getty Images

Hata hivyo, mapigano yanaendelea kusini mwa mji wa Uvira katika eneo la Makobola na milima ya Swima na Kasekezi katika tarafa ya Fizi, kati ya jeshi la Kongo, FARDC, wakishirikiana na Wazalendo dhidi ya waasi wa M23 wanaotaka kusonga mbele kuelekea mji wa Baraka.

Hali hiyo inazusha hofu katika jamii na kusababisha maelfu ya familia kukimbia makwao jambo ambalo Waziri Muyaya amekiri na kusikitikia. “Leo, tuna takwimu ya wakimbizi 200,000. Hali ni tete. Ni wazi, tutafanya sehemu yetu, kuhakikisha kwamba tunatoa makazi, na kuhakikisha wenzetu wanatunzwa vyema popote walipo. Kuna ujumbe umeenda Burundi na mwingine utawasili Tanzania kutathmini mahitaji na rasilimali zote. Lakini nadhani hapa, panahitajika uhamasishaji mkubwa zaidi. Ni lazima kuwe na amani kwani kitu bora tunachoweza kutoa kwa familia zilizohamishwa ni fursa ya kurudi nyumbani.”

M23 yaonya huenda ikatanua udhibiti hadi Katanga

To view this video please enable JavaScript, and consider upgrading to a web browser that supports HTML5 video

Wakati hayo yanajiri muungano wa AFC/M23 unaoungwa mkono na Rwanda, umetangaza mipango ya kupanua shughuli zake zaidi mashariki mwa Kongo.

Akizungumza wakati wa sherehe za kuadhimisha mwaka wa pili wa vuguvugu hilo, mratibu Corneille Nangaa amesema waasi hao wananuia kuongeza shughuli zao katika jimbo la Ituri, kaskazini mashariki na Katanga kusini mashariki.

Nangaa alilishutumu jeshi la Kongo na washirika wake Wazalendo kwa kuendeleza vurugu katika maeneo ya Masisi, Walikale, Fizi, Minembwe, na Mikenge.

Kundi la M23 liliiteka Uvira mapema mwezi huu bila upinzani kabla ya kutangaza kujiondoa kwa upande mmoja, jambo ambalo lilielezwa kama hatua ya kujenga imani katika kuunga mkono mchakato wa amani wa Doha. Lakini Kinshasa inasisitiza kuwa hatua hiyo ipo kwenye karatasi pekee.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *