Hata hivyo hakuna uamuzi rasmi uliochukuliwa kuhusu suala hilo na kuafikiana kulifanyia kazi badala ya mkopo wa pamoja. Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky amesema nchi yake iko tayari kwa mfumo wowote wa kutumia mali za Urusi zilizozuiwa lakini akasema angependelea zaidi pendekezo la mkopo kuliko kutumia mali za Urusi. Zelensky amezitaka nchi za Ulaya kuchukua uamuzi wa mwisho kabla ya mwaka huu kumalizika. Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron ametoa pia wito wa kufanikisha mpango huo.
Kwa sasa tunahitaji kuwapa Waukraine uhakika wa kifedha ili kuendelea na juhudi zao za vita. Huu ndio uamuzi tunaopaswa kufanya. Tume ya Ulaya imewasilisha mapendekezo kadhaa, na majadiliano muhimu yameanza kuhusu matumizi ya mali za Urusi zilizozuiliwa. Ni muhimu kuwaleta pamoja wadau wote, na tutafikia msimamo utakaotuwezesha kufanya uamuzi,” alisema rais Macron.
Aidha, Benki Kuu ya Urusi imesema leo kuwa itazishtaki benki za Ulaya katika mahakama za Urusi kuhusiana na mipango ya kuzitumia mali za Urusi zilizozuiwa kuifadhili Ukraine.
Wakati huohuo, mkutano wa Alhamisi wa viongozi wa Umoja wa Ulaya umejadili pia masuala mengine yaliyosababisha mvutano, yakiwemo majadiliano ya mkataba wa biashara kati ya Umoja wa Ulaya na nchi za Amerika ya Kusini kuhusu mauzo ya mazao ya kilimo. Hatua hiyo inapinga vikali na wakulima wa Ulaya, ambao wameandamana leo Alhamisi mjini Brussels.