Taarifa kutoka katika chombo cha habari cha umma nchini Korea Kaskazini zimeripoti kuwa kiongozi wa taifa hilo Kim Jong Un ameagiza ‘kuongeza’ na kuboresha uzalishaji wa makombora ya nchi hiyo mwaka ujao, pamoja na ujenzi wa viwanda zaidi ili kukidhi mahitaji yanayoongezeka. Katika ziara yake katika viwanda vya silaha akiwa na maafisa waandamizi, Shirika la Habari la Korea (KCNA) limesema Kim ameagiza viwanda hivyo kukidhi ‘mahitaji yanayotarajiwa katika uendeshaji wa vikosi vya makombora na mizinga vya taifa’. Wachambuzi wanasema hatua hii inalenga kuboresha uwezo wa mashambulizi ya uhakika, kuipa changamoto Marekani pamoja na Korea Kusini, na kujaribu silaha kabla ya uwezekano wa kuziuza kwa Urusi. Kimsingi chama tawala cha Korea Kaskazini, Chama cha Wafanyakazi wa Korea, kinatarajiwa kufanya kongamano lake la kwanza katika nusu ya muongo mapema mwaka 2026, ambapo watunga sera watajadili mipango ya maendeleo ya kiuchumi na kijeshi kwa miaka mitano ijayo.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *