LICHA ya maafande wa Mashujaa kuachana na beki wa kati, Abdulmalik Zakaria aliyejiunga Singida Black Stars, uongozi wa kikosi hicho umeweka wazi kuondoka kwa mchezaji huyo si pengo tofauti na eneo la beki wa kulia ambako kwa sasa wanasaka mtu wa kuja kuimarisha eneo hilo.

Abdulmalik aliyejiunga na Mashujaa akitokea Namungo Julai 19, 2024, amefikia makubaliano ya kuondoka katika kikosi hicho cha maafande kwa ajili ya kupata changamoto mpya, huku uongozi wa timu hiyo ukihaha kupata beki mwingine ila wa kulia.

Akizungumza na Mwanaspoti, Mwenyekiti wa Mashujaa, Meja Abdul Tika, amesema wanaheshimu uamuzi wa mchezaji huyo kuondoka ndani ya kikosi hicho, ingawa nafasi anayocheza sio pengo kubwa sana kwao, kutokana na wachezaji wengi walio kikosini.

“Sehemu kubwa tunayopambana nayo katika dirisha hili dogo ni kuongeza nguvu eneo la beki wa kulia kwa sababu baada ya kuondoka, Omary Kindamba kumekuwa na changamoto, licha ya baadhi ya wachezaji kucheza nafasi hiyo,” amesema Abdul Tika.

Tika amesema baada ya kuondoka kwa Abdulmalik wengi wanatarajia asake mbadala, ingawa kutokana na wingi wa nyota wanaocheza nafasi hiyo wataendelea kuboresha kwingine.

Kindamba aliyejiunga na Gunners ya jijini Dodoma inayoshiriki Ligi ya Championship msimu huu, ndiye aliyekuwa beki wa kulia wa kutumainiwa wa kikosi hicho, licha ya Samson Madeleke kucheza pia eneo hilo na wakati mwingine beki wa kati.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *