DAR ES SALAAM: MKURUGENZI Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI), Dk Peter Kisenge amesema idadi ya watalii wanaotibiwa katika tawi la Oyster Bay Plaza imeongezeka kutoka wagonjwa 10 hadi kufikia 120 kwa mwezi jambo linalochochea utalii tiba kuendelea kukuwa kwa kasi nchini.
Amesema watalii tiba hao wanatokea zaidi nchi 20 ikiwemo Comoro, Malawi, China, Poland, Congo, England, Msumbiji, Misri,Ujerumani na Italia baadhi yao wakiwa wamekuja kwa ajili ya utalii na wengine wakija moja kwa moja kutibiwa nchini.
Dk Kisenge alisema hayo jana wakati wa maadhimisho ya mwaka mmoja tangu kuanzishwa kwa huduma ya matibabu ya moyo katika tawi la Oyster Bay Dar es Salaam.
Amesema kupitia utalii tiba katika tawi hilo wamekusanya Sh bilioni 1 kwa mwenzi fedha zinazokwenda kugharamia matibabu ya wagonjwa wasiokuwa na uwezo hasa upasuaji wa watoto wenye matundu kwenye moyo.

Amesema kupitia utalii tiba katika tawi hilo wamekusanya Sh bilioni 1 kwa mwenzi fedha zinazokwenda kugharamia matibabu ya wagonjwa wasiokuwa na uwezo hasa upasuaji wa watoto wenye matundu kwenye moyo.
‘’Kliniki hii imekuwa na tija kwenye taasisi ya moyo kwa sababu tumepata watalii wengi ambao tunaita utalii tiba wamekuja kutibiwa hapa na fedha zilizopatikana zimetumika kuwasaidia wagonjwa wasiokuwa na uwezo na taasisi yetu inasamehe zaidi ya Sh milioni 200 kwa mwezi,’’amesema Dk Kisenge.
Ameeleza kuwa ongezeko hilo la utalii tiba limetokana na upatikanaji wa huduma bora za kibingwa zinazotolewa katika tawi hilo baada ya Serikali ya Awamu ya Sita kuboresha uwekezaji wa miundombinu ya utoaji huduma pamoja na ununuzi wa vifaa vya kisasa ikiwemo mitambo inayotumia akili unde.
Amesema kupitia kituo hicho wamefanikiwa kupunguza msongamano wa matibabu katika tawi la Muhimbili, Temeke, Kawe na Dar Group ambako awali walikuwa wakitumia muda mrefu kupata matibabu lakini sasa huduma hizo hutolewa chini ya saa moja wagonjwa wenye bima,wasio na bima na wasiokuwa na uwezo wa kumudumu gharama za matibabu.

‘’Nia ya taasisi ni kuhakikisha kila Mtanzania asiyekuwa na uwezo anatibiwa lakini pia tumefanikiwa kupunguza watu kutibiwa nje,tuna vifaa vya kumfuatilia mgonjwa akiwa nyumbani kupitia shuka maalumu ambalo linaangalia mapigo yake ya moyo,presha na tunaweza kumuona na tukamuhudumia akiwa nyumbani kwakwe,’’amesema.
Naye msimamizi wa kituo cha JKCI tawi la Oyster Bay, Smita Bhalia amesema kuwa tawi hilo lilipozinduliwa Desemba 27,2024 walikuwa wanahudumua wagonjwa 250 kwa mwezi lakini hadi kufikia Desemba 27, mwaka huu kwa mwezi wanahudumia wagonjwa 900.
Amesema tawi hilo linatoa huduma za matibabu kwa magonjwa mbalimbali ikiwemo matibabu ya lishe,kupunguza uzito,maumivu ya muda mrefu ya viungo pamoja na matibabu ya mgonjwa aliyepooza.