
Uhusiano wa Harmonize na Kajala Masanja umekuwa na matukio mengi ya panda shuka ambayo kwa miaka zaidi ya minne sasa yamekuwa yakigonga vichwa vya habari na kuvutia usikivu wa mashabiki.
Sasa kwa kulitambua hilo, tunakuletea mtiririko wa matukio ya urafiki hadi uhusiano wao tangu walipoanzana, kuachana, kurudiana na hadi sasa ambapo wamerudiana kwa mara nyingine tena.
Agosti 2017: Harmonize anamtaja Kajala
Katika wimbo wa WCB Wasafi, Zilipendwa (2017), ndipo Harmonize alimtaja Kajala kwa mara ya kwanza ila haikujadiliwa, wakati huo uhusiano wao ulikuwa haujulikani ila hatuwezi kusema ilikuwa bahati mbaya.
“P-Funk Kajala (zililipendwa). Onyango na Jangala (zilipendwa),” aliimba Harmonize katika wimbo huo uliokutanisha wasanii wengine kama Diamond Platnumz, Rich Mavoko, LavaLava, Queen Darleen, Rayvanny na Mbosso.
Kwa mujibu wa mahojiano mapya ya Kajala, uhusiano wao ulianza kitambo wakati Paula akiwa sekondari na aliwahi kumlipia ada akiwa kidato cha pili, hivyo huenda Harmonize alimaanisha jambo katika wimbo huo.
Februari 2021: Wanathibitisha kuwa pamoja
Baada ya tetesi za muda mrefu huku wakiteka mazungumzo katika mitandao ya kijamii, hatimaye Februari 2021, Harmonize na Kajala waliweka hadharani uhusiano wao wakionekana pamoja katika matukio kadhaa.
Hatua hiyo ilikuja siku chache baada ya Harmonize kusitisha ziara yake kimuziki (In The Club Tour) kwa madai kuwa hali yake ya kiafya sio nzuri. Ziara hiyo ilianzia Mwanza na ilipangwa kupita mikoa mingi nchini.
Kusitishwa kwa ziara hiyo kukatoa fursa kwa uhusiano wao kukua mbele ya macho ya umma huku kukiwa na mjadala uliojikita katika tofauti ya umri wao (takribani miaka 10), mjadala ambao kwa sasa hausikiki tena.
Februari 2021: Ugomvi mzito unaibuka
Wakati uhusiano ukiendelea kupamba moto, ghafla linatokea tukio la aibu. Ni video za Harmonize zinazodaiwa alikuwa akimshawishi binti wa Kajala, Paula ili kuwa naye kimapenzi ilihali yupo na mama yake!
Ni sakata lililowafikisha wote polisi akiwamo Rayvanny ambaye wakati huo alikuwa na Paula, uhusiano ambao ulikuja kuisha kwa ugomvi huku Kajala akitupa lawama kwa Hamisa Mobetto akidai ndiye aliwakutanisha.
Hata hivyo, katika mfululizo wa vipindi vyao, Behind The Gram, Paula alikiri kwa kinywa chake akidai kuwa anamchukia Harmonize kwa sababu alimtongoza wakati anajua bado ana uhusiano na Kajala (mama yake).
Novemba 2021: Harmonize ana-move on!
Akiwa anaendelea na ziara yake ya muziki nchini Marekani hapo Novemba 2021, Harmonize akamtambulisha Briana kutokea Australia kama mpenzi wake mpya, na baada ya ziara hiyo alikuja naye Bongo.
Hata hivyo, uhusiano huu ulidumu kwa muda wa miezi mitano tu, hivyo waliachana Machi 2022, ukiwa ni uhusiano wa nne wa Harmonize uliowekwa hadharani kuvunjika.
Ikumbukwe tayari alikuwa ameshaachana na Kajala, Jacqueline Wolper na Sarah kutokea Italia ambaye walifunga hadi ndoa ila nayo ilivunjika kwa madai ya usaliti baada ya kudumu kwa takribani mwaka mmoja.
Aprili 2022: Harmonize anamlilia Kajala
Baada ya kuachana na Briana, Harmonize alianza kutuma mfululizo wa jumbe kupitia Insta Story akieleza kuwa anahitaji kurudiana na Kajala, huku wapambe wake mbambali nao wakimsaidia suala hilo.
Harmonize alieleza kuwa watu wanaweza kumuona mwenye furaha lakini sivyo, anachotaka ni familia yake kurejea nyumbani. Familia hiyo ni Kajala na binti yake, Paula ambao alikuwa akiishi nao hapo awali.
Hatua hiyo ilikuja baada ya Harmonize kutoa wimbo, Mtaje (2021) ambao ulikuwa maalum kwa ajili ya kumbembeleza Kajala. Moja ya mistari yake inasema; “mwambieni mwanangu Paula mimi nampenda mamaye.”
Juni 2022: Kajala anavishwa pete
Harmonize alifanikiwa kumshawishi Kajala arejee kwake, jambo ambalo wengi hawakutegemea kutokana na yale yalitokea kati yao lakini hayo ndio mapenzi, muda mwingine yanaonyesha maajabu yake.
Awamu hii Harmonize alikuja kiutofauti kidogo akionyesha kuwa amedhamiria kufanya kitu, ndipo akachukua hatua ya kumvisha Kajala pete ya uchumba, hatua ambayo ilimtoa machozi mrembo huyo.
Tukio hilo ambalo lilifanyika Juni 25, 2022 katika hoteli ya Serena, Dar es Salaam, Paula naye alihudhuria, na huu ulikuwa ni uthibitisho kuwa amesamehe yote aliyodai kutendewa na yupo tayari kwa ukurasa mpya ujao.
Septemba 2022: Kajala katika video
Kwa mara ya kwanza Kajala anatokea katika video ya Harmonize, nayo ni ya wimbo, Nitaubeba (2022), katika video hiyo walivalia kama bwana na bibi harusi wenye furaha kubwa baada ya kufunga ndoa.
Katika wimbo huu, Harmonize anamwambia mke wake kuwa kabla ya kulala, humuomba Mungu amlinde na kumtunza, kwa sababu yeye ni pacha wake wa maisha.
Anaeleza kuwa atakuwa naye bega kwa bega katika nyakati zote – wakati wa shida na tabu, furaha na huzuni, shibe na njaa. Wimbo huu unaakisi upendo wa dhati, uaminifu na mshikamano wa kweli katika ndoa.
Itaendelea…