Marekani imemteka nyara Rais wa Venezuela Nicolas Maduro siku ya Jumamosi, Januari 3, ikimtuhumu kwa miezi kadhaa ya kung’ang’ania madaraka kinyume cha sheria na kuwezesha biashara ya dawa za kulevya. Katika mkutano na waandishi wa habari, Donald Trump amebainisha kwamba hali hiyo inaweza kuwakumba viongozi wengine wa dunia.

Imechapishwa:

Dakika 3 Wakati wa kusoma

Matangazo ya kibiashara

Washington haikuwa imetumia uingiliaji kati wa moja kwa moja huko Amerika Kusini tangu uvamizi wa Panama mwaka wa 1989 uliowezesha kumng’oa mamlakani kiongozi wa kijeshi Manuel Noriega. Katika saa za mapema za Jumamosi, Januari 3, vikosi maalum vya Marekani viliingilia kati, huku kukiwa na milio ya risasi, katika mji mkuu Caracas na kumteka nyara rais wa Venezuela na mkewe.

Nicolás Maduro na mkewe sasa watakabiliwa na haki ya Marekani, huku mashtaka ya “ugaidi wa dawa za kulevya” na uingizaji wa kokeni nchini Marekani yakiwa yamewasilishwa.

Wakati wa mkutano na waandishi wa habari uliofanyika na Waziri wa Mambo ya Nje Marco Rubio, Waziri wa Ulinzi Pete Hegseth, na Mkuu wa majeshi ya Marekani Jenerali Dan Caine, Donald Trump alielezea kwa shauku “mafanikio” ya operesheni ya jeshi la Marekani nchini Venezuela. Pia aliwatishia viongozi wengine, haswa mwenzake wa Colombia Gustavo Petro: “Anamiliki viwanda ambapo anatengeneza kokeini. […] Anatengeneza kokeini na kuisafirisha hadi Marekani, kwa hivyo lazima awe mwangalifu,” alitangaza.

Cuba pia iko katika njia panda za utawala wa Trump. “Kama ningeishi Havana na ningekuwa sehemu ya serikali, ningekuwa na wasiwasi kidogo,” alisema Marco Rubio, akiongeza kuwa nchi hiyo ni “janga” na “inaongozwa na wanaume wasio na uwezo na wazee.”

“Marco Rubio alijenga taaluma yake ya kisiasa kwa nia ya mabadiliko ya utawala huko Havana na Caracas,” Thomas Posado, mhadhiri wa ustaarabu wa kisasa wa Amerika Kusini katika Chuo Kikuu cha Rouen, alituambia. “Kituo chake cha uchaguzi kiko Florida, ambapo alichaguliwa kutokana na jamii za Amerika Kusini zenye chuki dhidi ya ukomunisti—hasa Wakuba na Wavenezuela. Aina hii ya siasa itaongeza umaarufu wake katika jamii hizi.” 

“Ni vigumu operesheni kama hiyo kutokea tena”

Wakati wa mkutano huo na waandishi wa habari, rais wa Marekani pia alirejelea vitisho vyake dhidi ya utawala wa Iran ikiwa ungehusika na vifo vya waandamanaji, huku nchi ikitikiswa na wimbi kubwa la maandamano.

Je, viongozi hawa wanapaswa kuogopa kuwa “wanaofuata kwenye orodha”? Ingawa utawala wa Iran tayari umetikiswa na hatua kubwa ya Marekani—mashambulizi kwenye maeneo yake ya nyuklia mwezi Juni mwaka uliyopita—Bogotá haipaswi kuwa na wasiwasi kupita kiasi, kulingana na afisa wa zamani Guillaume Ancel, mwandishi wa blogu ya Ne pas souffrir (Usiumie).

Na hii ni kwa sababu mbili: “Ya kwanza ni kwamba mafanikio ya operesheni iliyofanywa na Wamarekani yalitegemea mshangao. Kila mtu alishangaa na sasa anajiuliza: ‘Waliwezaje kumteka nyara rais Maduro na mkewe katika nchi hii kubwa?'” Kwa sababu Venezuela ni nchi kubwa yenye jeshi lenye nguvu, na ilikuwa ikitarajia kuonyesha upinzani mkubwa—ingawa si wa aina hii—kutoka Marekani. Kwa hivyo, kuiga kuendesha operesheni kama hiyo dhidi ya Colombia haitawezekana.

“Kwa upande mwingine,” mtaalamu huyo ameongeza, “serikali ya Marekani haipaswi kupuuza siasa za ndani. Haikuwa imearifu Bunge, na sasa inalazimika kufanya hivyo. Ikiwa ilitaka kuanzisha uingiliaji kati mrefu zaidi, ingehitaji idhini ya Bunge. Tunakumbuka kwamba moja ya ahadi za kampeni za Donald Trump ilikuwa: ‘Nitakuwa rais ambaye hatatuongoza tena vitani. Ninapinga vita.’ Lakini alichofanya hivi punde ni kuanzisha operesheni ya kijeshi, vita dhidi ya Venezuela.”

Kuhusu Cuba, Thomas Posado pia haoni tishio lolote lililo karibu. “Kama angefanikiwa kumpindua Miguel Diaz-Canel huko Cuba, ingekuwa ushindi mwingine wa vita kwa Marco Rubio. Hivi sasa, kwa mtazamo wa kijeshi, mafanikio ya operesheni hii huko Venezuela tayari ni kama muujiza, na tunaweza kufikiria kwamba miujiza haitatokea tena. Hasa kwa kuwa mataifa ya Amerika Kusini sasa yanafahamu mbinu za utawala wa Trump. Kwa hivyo itakuwa ngumu zaidi kudhibiti vita tofauti.”

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *