Mashambulizi ya anga yaliyofanywa na Marekani dhidi ya Venezuela na kukamatwa kwa kiongozi wa nchi hiyo Nicolas Maduro mwishoni mwa wiki yamekosolewa na viongozi mbali mbali.

Umoja wa Mataifa umesema ni hatua inayohujumu waziwazi, msingi wa sheria ya kimataifa. Nchi za Afrika pia zimekosoa hatua ya Marekani.

Msemaji wa ofisi ya kusimamia  haki za binadamu ya Umoja wa Mataifa, Ravina Shamdasani amewaambia waandishi wa habari mjini Geneva kwamba hakuna taifa  ulimwenguni linapaswa kutumia vitisho au nguvu dhidi ya taifa jingine au kuingilia uhuru wa kisiasa wa nchi nyingine.

Shamdasani amezungumzia hali ya  Venezuela akisema hicho ndicho kinachotokea hivi sasa huku akiitolea mwito jumuiya ya Kimataifa kuungana pamoja na kutoa msimamo wa pamoja kuweka wazi kwamba kitendo kilichofanywa na Marekani ni kinyume na sheria ya Kimataifa iliyopitishwa na wanachama wa Umoja wa Mataifa.

Kikao cha dharura cha baraza la usalama la UN kuhusu Venezuela
Kikao cha dharura cha baraza la usalama la UN kuhusu VenezuelaPicha: Kyodo/picture alliance

Nchi za Afrika jana zilijitokeza waziwazi katika kikao cha baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kukemea kilichofanywa na Marekani nchini Venezuela.

Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo kama mwanachama wa baraza hilo wanaoliwakilisha bara la Afrika sambamba na Liberia na Somalia wamezungumzia wasiwasi wao kuhusu hali hiyo ya kuingiliwa kwa Venezuela.Maduro afikishwa Mahakamani huko Marekani

Balozi wa kudumu wa Liberia katika Umoja wa Mataifa  Lewis Garseedah Brown II, akitowa msimamo huo wa pamoja kwa niaba ya Umoja wa Afrika aliweka mkazo juu ya kuheshimiwa sheria ya Kimataifa.

”Nchi tatu za Afrika A3 zinabakia imara katika ahadi zake kwenye misingi ya sheria ya Kimataifa ikiwemo kushimu kikamilifu uhuru wa mipaka na kila taifa kuwa na uhuru wa kudhibiti mipaka yake,kama ilivyofafanuliwa kwa kina katika mkataba wa Umoja wa Mataifa kwa kuzingatia  maslahi ya uthabiti wa kikanda na amani ya Kimataifa”

Nchi hizo tatu zinazofahamika kama A3 ambazo sio wanachama wa kudumu wa baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, katika tamko lao hilo la pamoja lenye msimamo wa Umoja wa Afrika pia zimetowa mwito wa kuzingatiwa amani na kupatikana mchakato endelevu utakaoleta suluhisho utakaosimamiwa na Wavenezuela wenyewe na kuungwa mkono na Jumuiya ya Kimataifa.

Nicolas Maduro alikamatwa Januari 3 mjini Caracas na wanajeshi wa Marekani
Nicolas Maduro alikamatwa Januari 3 mjini Caracas na wanajeshi wa MarekaniPicha: Giorgio Viera/AFP/Getty Images

Jumuiya ya kiuchumi ya nchi za Kanda ya Afrika Magharibi ECOWAS, nayo pia imetowa msimamo wake ikisema inafuatilia kwa wasiwasi mkubwa hali inayoendelea katika jamhuri ya Venezuela.

Pamoja na kutambuwa haki ya Marekani ya kukabiliana na uhalifu wa Kimataifa ikiwemo Ugaidi na bishara ya mihadarati,Ecowas imeweka wazi kwamba ingependa kuikumbusha Jumuiya ya Kimataifa kuhusu wajibu wao wa kuheshimu uhuru wa mipaka wa mataifa ya wengine.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *