
Angalau wanajeshi wanane waliuawa siku ya Jumapili katika Jimbo la Borno, kaskazini mashariki mwa Nigeria, wakati bomu lililotegwa kando ya barabara lilipolipuka baada gari lao la kivita lilipokuwa likipita, chanzo cha kijeshi kimelambia shirika la habari la AFP.
Imechapishwa:
Dakika 2 Wakati wa kusoma
Matangazo ya kibiashara
Ripoti ya hali iliyoandaliwa kwa ajili ya Umoja wa Mataifa na iliyoonekana na shirika la habari la AFP imeripoti idadi ya vifo kutokana na mlipuko huo kuwa tisa, ikibainisha kwamba wapiganaji kutoka Islamic State Afrika Magharibi (ISWAP) “walilipua” kifaa hicho wakati wanajeshi “waliposimamishwa (…) barabarani kati ya Gubio na Damasak.”
Nigeria, yenye watu wengi zaidi barani Afrika inakabiliwa na uasi wa wanajihadi, hasa uliojikita kaskazini mashariki, ukiongozwa na Boko Haram na kundi pinzani lake, Islamic State katika Afrika Magharibi (ISWAP). Ingawa Jimbo la Borno ndilo kitovu cha uasi huu wa wanajihadi, mlipuko huko Gubio, uliosababishwa na kifaa cha kulipuka, ulitokea katika “eneo lisilo la kawaida” la aina hii ya bomu, ikibainika kwamba “ISWAP inapanua eneo lake la operesheni na inaweza kuwa inaweka vifaa vya kulipuka vilivyotengenezwa kienyeji mbali na maeneo yake ya kawaida,” kulingana na ripoti hiyo.
Chanzo cha kijeshi kilichozungumza kwa sharti la kutotajwa jina kimebainisha kuwa wanajeshi wanane waliuawa. Hata hivyo, vikosi vya kijeshi vya Nigeria bado havijathibitisha rasmi shambulio hili la wanajihadi. Chanzo hiki cha kijeshi kimeripoti shambulio la kuvizia lililofanywa na wapiganaji wa ISWAP, ambapo kifaa cha kulipuka kiligonga gari linalostahimili mabomu na linalolindwa na mashambulizi ya kuvizia (MRAP).
Zaidi ya watu 40,000 wamekufa kaskazini mashariki mwa nchi tangu 2009
Kulingana na takwimu za Umoja wa Mataifa, uasi wa Kiislamu nchini Nigeria umewaua zaidi ya watu 40,000 na kusababisha takriban watu milioni 2 kaskazini mashariki mwa nchi kutoroka makazi yao tangu ulipoanza mwaka wa 2009. Mgogoro huo umeenea hadi nchi jirani, ikiwa ni pamoja na Niger, Cameroon, na Chad. Mlipuko wa Jumapili ulikuja siku moja baada ya kifaa cha kulipuka cha ISWAP kuwajeruhi wanajeshi kadhaa kwenye mhimili wa Wajiroko-Azir katika wilaya ya Damboa, Jimbo la Borno, kulingana na ripoti hiyo, ambayo pia imebainisha kuibuka tena kwa shughuli za ISIS katika Jimbo la Borno mwezi Desemba.
Katika miezi ya hivi karibuni, Marekani imekosoa kushindwa kwa Nigeria kukomesha vurugu hizo. Rais wa Marekani Donald Trump alilaani madai ya “mateso” dhidi ya Wakristo—hoja ambayo kwa muda mrefu ilitumiwa na mrengo wa kulia wa kidini wa Marekani—huku mauaji hayo yakiwalenga Wakristo na Waislamu bila kubagua. Shutuma hizi za Marekani zinakanushwa vikali na serikali ya Nigeria na wachambuzi huru. Marekani ilianzisha mashambulizi ya anga ya kushtukiza siku ya Krismasi, ikidai kuwalenga wanajihadi waliohusishwa na kundi la Islamic State. Abuja ilisema kwamba ilidhinisha mashambulizi hayo.