Mchina adakwa na mabilioni ya fedha DarMchina adakwa na mabilioni ya fedha Dar

JESHI la Polisi Tanzania limesema linafuatilia na kuchunguza picha mjongeo inayomwonesha raia wa kigeni mwenye asili ya China akiwa na mifuko ya sandarusi iliyojaa fedha za ndani na za kigeni.

Msemaji wa Jeshi la Polisi, David Misime ameliambia gazeti la HabariLEO kuwa baada ya uchunguzi kukamilika atatoa taarifa kamili kuhusu tukio hilo.

“Nilikuwa kwenye kikao ndio nimetoka na nimeiona hiyo picha mjongeo. Uchunguzi umeanza na tunaifuatilia ili kupata taarifa kamili kisha kuitoa kwa vyombo vya habari kueleza tukio hilo,” alisema Misime.

SOMA: Polisi yatangaza nafasi mpya za ajira

Picha mjongeo hiyo ilisambaa jana katika mitandao ya kijamii ikimuonesha raia huyo wa kigeni akiwa amezungukwa na watu wanaohisiwa kuwa polisi waliovaa kiraia wakimpa maelekezo ya kuzitoa fedha hizo kutoka katika mifuko mitatu.

Tukio hilo linasemekana kutokea nyumbani kwake eneo la Oysterbay, Mtaa wa Mazengo nyumba za Phoneix.

Taarifa zilizosambaa katika mitandao ya kijamii zinasema majirani na viongozi wa Serikali ya Mtaa ya Oysterbay ndio waliotoa taarifa kwa vyombo vya usalama na kufanikisha kukamatwa kwake.

Kwa mujibu wa taarifa hizo, raia huyo akiwa na wenzake hutoka nyumbani kwao majira ya saa 1:30 usiku na kurudi saa 10:00 alfajiri wakiwa na mifuko iliyojaa fedha.

Taarifa hiyo inaeleza kuwa baada ya kukamatwa watuhumiwa hao walikutwa na fedha taslimu ambazo ni Dola za Marekani na Shilingi za Tanzania ambazo jumla yake ni zaidi ya Sh bilioni sita ambazo zimefichwa ndani ya nyumba namba 317 ghorofa ya tatu

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *