Ushiriki wa wanawake katika siasa za Uganda umekuwa wa dhati katika chaguzi zilizopita ambapo angalau mmoja wao aligombea urais na kusawazisha kinyang’anyiro hicho kwa kuwakilisha jinsia hiyo. Ila
safari hii, kati ya wagombea wanane wa kiti cha urais hakuna mwanamke hata mmoja. Kulingana na wachambuzi wa masuala ya kisiasa na watu mbalimbali, wanawake ambao wangetegemewa kugombea urais wana sababu mbalimbali za kutothubutu.
Hata hivyo wanawake wengine wanaelezea kuwa uchaguzi wa Uganda hauna uwazi na si huru na wa haki kuanzia maandalizi yake hadi kutangazwa kwa mshindi. Hata hivyo kulingana na mchambuzi Akol Amazima, mfumo dume ungali unatawala katika mazingira ya kisiasa hata katika mataifa ambayo yanadhaniwa kuwa na demokrasia iliyokomaa.
Wanawake waliowahi kujitokeza walikuwa wagombea huru
Aidha, kuna mtazamo kuwa wanawake hawajapewa nafasi za uongozi hata katika vyama vya siasa ambavyo ndiyo kawaida humdhamini mgombea na kumpa usaidizi wa kutosha katika kampeni zake.
Wengi wa wanawake waliojitokeza kugombea katika chaguzi zilizopita walikuwa wagombea huru bila udhamini wa vyama. Mmoja tu Beti Kamya aliyegombea mwaka 2011 alikuwa na chama chake cha muungano wa majimbo UFA. Lakini mara tu baada ya kushindwa katika uchaguzi huo alikiacha chama chake alichokianzisha na kujiunga na serikali yaRais Yoweri Museveni ambapo alipewa nafasi ya uwaziri na baadaye kuwa mkaguzi mkuu wa serikali hadi majuzi alipokosa kuongezewa awamu nyingine.
Winnie Byanyima alipewa nafasi kubwa ya kugombea
Miongoni mwa wanawake tajika wanaoelezewa kuwa wangeweza kugombea urais nchini Uganda ni Mhandisi Winnie Byanyima, mke wa mwanasiasa mashuhuri Dkt Kizza Besigye ambaye kwa sasa yumo gerezani.
Hii ni kutokana na tajriba yake tangu alipokuwa na kundi la NRA lililomleta rais Museveni madarakani;wengine ni Sarah Birete mwanaharakati wa haki za binadamu ambaye hivi majuzi alikamatwa na kuzuiliwa katika mazingira tata; Miria Matembe mwanaharakati wa siku nyingi wa haki za wanawake na pia Winnie Kiiza aliyewahi kuwa kiongozi wa upinzani bungeni.
Licha na wanawake kutogombea urais, kuna idadi kubwa ambao wameshuhudiwa wakiandamana na kuwapigia debe wagombea wao wa urais. Dkt Lina Zedriga makamu wa rais wa chama cha NUP, spika wa bunge Anita Among pamoja na mke wa rais Museveni Janet Kataha wameonyesha ushiriki mkubwa katika kampeni za wagombea wa vyama vyao.