Siku chache tu kabla ya uchaguzi wa Januari 15, waandishi kadhaa wa habari nchini Uganda wanasema wanafanya kazi katika hali ya hofu. Shambulio dhidi ya mwandishi wa habari Ivan Mbadi siku ya Jumatatu, Januari 5, alipokuwa akiripoti kampeni ya kiongozi wa upinzani Bobi Wine, linaonyesha mwenendo mbaya kwa miaka mingi na watetezi wa uhuru wa vyombo vya habari.

Imechapishwa:

Dakika 4 Wakati wa kusoma

Matangazo ya kibiashara

Katika video iliyosambaa sana kwenye mitandao ya kijamii, Ivan Mbadi anaonekana amebanishwa kwenye gari, akijaribu kujitoa katika hali hiyo, kisha ameketi, akionekana kuchanganyikiwa. Baadaye, hospitalini, anarekodiwa akionekana dhaifu, akiwa amewekewa bandeji shingoni. Kulingana na wale walio karibu naye, alilengwa baada ya kupiga picha maafisa wa polisi wakirusha gesi ya machozi dhidi ya ummati wa watu.

Kwa Keneth Kitambula, afisa wa programu katika Kituo cha Haki za Binadamu nchini Uganda, shambulio hili si tukio la pekee. “Nchini Uganda, waandishi wa habari wanatishiwa na kufanyiwa vurugu kila siku.” Ivan alikuwa “mwenye bahati” kwa sababu alikuwa akiandamana na Bobi Wine, ambaye timu yake ina ufanisi mkubwa katika kurekodi dhuluma hizi. Lakini katika ngazi ya chini, katika maeneo ya vijijini, tuna waandishi wa habari waliokamatwa, wakati mwingine wakiteswa, bila hali yao kuwekwa hadharani.

Nchi yenye nafasi ndogo kwa uhuru wa vyombo vya habari

Kulingana na Shirika la Waandishi wa Habari Wasio na Mipaka (RSF), Uganda inashika nafasi ya 143 kati ya 180 kwa uhuru wa vyombo vya habari.

Kielezo cha mwaka 2024 cha Mtandao wa Haki za Binadamu kwa Waandishi wa Habari (HRNJ) kinaorodhesha visa 110 vya vurugu dhidi ya waandishi wa habari. “Hali ya kisiasa imekuwa ikiathiri kazi ya waandishi wa habari nchini Uganda. Wanapitia mazingira magumu, yaliyogawanyika kati ya usalama wao na wajibu wao wa kutoa taarifa,” anaelezea Keneth Kitambula.

Hata hivyo Katiba inahakikisha uhuru wa kujieleza (Ibara ya 29) na haki ya kupata taarifa (Ibara ya 41). Lakini kwa msingi, “sheria hizi hupuuzwa kwa kiasi kikubwa na vikosi vya usalama.”

Kawempe Kaskazini, maabara ya ukandamizaji

Uchaguzi mdogo wa Kawempe Kaskazini mwezi Machi mwaka uliyopita unabaki akilini mwa kila mtu. Waandishi wa habari walipigwa na vifaa vyao kuharibiwa.

Canary Mugume, mwandishi wa habari wa uchunguzi wa televisheni ya NBS Television, alikuwepo siku hiyo. “Tumeona uwepo wa vikosi vya usalama, lakini hii haikuwa hali ya kawaida: vifaru mitaani, uwepo mkubwa wanajeshi.” Kisha hali ikawa mbaya zaidi. “Nilipiga picha ya wanajeshi wakiwachukua waandishi wa habari kwa nguvu. Mmoja wao aliponiona, alinifuata kwa kasi na kunitishia. Niliinua mkono wangu kwa kujisalimisha. Kwa muda wa sekunde thelathini, nilidhani maisha yangu yamekwisha.”

Aliporudi kwenye chumba cha habari, aligundua kuwa wenzake kadhaa walilazwa hospitalini, wengine wakiwa na majeraha ya kihwabi, kwenye goti, au mgongoni.

Waandishi wa habari wanaoripoti kampeni za upinzani walengwa

Kwa mujibu wa Keneth Kitambula, hatari ni kubwa sana kwa wale wanaoripoti habari za upande upinzani, haswa wakati wa kampeni za Bobi Wine, lakini pia hapo awali kwa Kizza Besigye. “Kimsingi ni waandishi wa habari wanaoripoti habari za upande wa upinzani ambao wanalengwa.”

Baadhi ya vyumba vya habari pia vinazuiliwa moja kwa moja. Nation Media Group – ambayo inamiliki Daily Monitor na NTV, miongoni mwa vingine – imepigwa marufuku na Rais Museveni kuripoti mikutano yake. Bunge pia limewazuia waandishi wake kuhudhuria vikao.

Larry Madowo, taarifa potofu, na kudhibiti habari

Hata waandishi wa habari wa kimataifa sasa wameathiriwa. Mwandishi wa habari wa CNN Larry Madowo alipuliziwa gesi ya machozi alipokuwa akiripoti kampeni ya Bobi Wine.

Baada ya kutuma ujumbe kwenye Twitter kwamba “gesi ya machozi ya Uganda ina ladha tofauti,” alifanyiwa kampeni ya kuchafuliwa mtandaoni. Video hiyo ilisambaa, ikidai kwamba rais Museveni alimzuia kuingi nchini. “Hii inafanya mazingira halisi ya hofu. Wakati CNN, chombo cha habari cha kimataifa, kinalengwa, serikali hutuma ujumbe wazi kwa waandishi wa habari wa ndani: ‘Ikiwa tunaweza kuwafanyia hivi wanahabari wa kigeni, fikirieni tunachoweza kuwafanyia nyinyi waandishi wa Uganda.'”

Shinikizo hili husababisha baadhi ya habari kutopasishwa kupita. “Waandishi wa habari wanasema: Sitaandika habari hii, sitaki kuhatarisha maisha yangu. Hii inafanya habari za uchaguzi kuwa ngumu zaidi,” anasema Keneth Kitambula.

Uamuzi wa mahakama ambao haujazingatiwa

Mnamo mwaka 2024, Mahakama Kuu ya Uganda iliamua kwamba mashambulizi dhidi ya waandishi wa habari yalikuwa kinyume cha katiba. Lakini kwa watetezi wa uhuru wa vyombo vya habari, ukosefu wa vikwazo halisi huchochea hisia ya kutokujali.

Kwa mujibu wa Canary Mugume, hati tayari imeandikwa: “Kuanzia Kawempe mwaka wa 2021 hadi mashambulizi ya kampeni hii, kila kitu kinaandaa mazingira kwa wiki ijayo. Huenda tukawaona waandishi wa habari wengi wakishambuliwa kuliko hapo awali.”

Licha ya matukio hayo, anakataa kusalimu amri: “Ni wajibu wetu. Tukikubali, kila kitu kitafanyika kwa siri. Kuwahabarisha raia ndiyo njia pekee ya kuwaruhusu raia kufanya maamuzi sahihi. Hivi ndivyo tunavyochangia, kwa demokrasia.”

RFI, imejaribu kuwatafuta viongozi wa Uganda hawakujibu.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *