DESEMBA 2, 2025 wakati anahutubia Wazee wa Dar es Salaam na Watanzania kwa ujumla, Rais Samia Suluhu Hassan alisisitiza jukumu muhimu la wazazi na walezi kushirikiana na kuelimisha watoto kama familia.

Maneno ya Rais Samia yanaibua tafakari na kunifanya nifikirie kuwa, kama wote tungetimiza majukumu yetu kikamilifu kama wazazi, baadhi ya vijana walioshiriki machafuko yaliyotokea siku ya Uchaguzi wa Oktoba 29, 2025 wasingeshiriki uhalifu huo.

Haraka maneno hayo yananifanya nihitimishe kuwa, nidhamu na mtazamo chanya kwa watoto tuliopewa na Mungu, ni mambo ambayo hayajitokezi tu kama matokeo ya ushawishi wa nje, bali huundwa kupitia mwingiliano wa mifumo ya malezi na mchakato wa kifamilia na kijamii.

Wazazi hufundisha nidhamu kwa ubora zaidi kwa kuanzisha taratibu, kanuni na matokeo yanayotekelezwa vyema, badala ya kutoa hotuba na maelezo marefu makosa yanapotokea. Kijana anapokulia katika mazingira suala la muda, majukumu na mipaka yake vinatabirika ikiwa ni pamoja na kuamka mapema, kufanya kazi za nyumbani na kusimamia kazi za shule, hujenga nidhamu hiyo na kuwa utaratibu wa maisha wa kila siku.

Mtaa hufundisha mikakati ya haraka ya ‘kujikimu’ ambayo si mara zote huwa njia bora. Familia kama mhimili wa jamii humjenga kijana katika hali ya upangaji wa maisha, uwajibikaji na uundaji wa maadili yanayobainisha mema na mabaya, kujua wakati kufanya lililo jema na kuepuka mabaya kadiri mtu anavyokua.

Bila kuyumba na kimyakimya, hujenga tabia njema kwa ufanisi zaidi kuliko maneno na tabia mbaya kutoka katika ‘shule za mitaani.’ Kutafakari maneno ya Rais Samia kunanikumbusha kwamba malezi bora hufundisha kuwa, vitendo vina matokeo na pia, makosa ni masomo na si sababu za kulaumu.

Vijana wanapotakiwa kurekebisha makosa yao, kuomba msamaha, au kujaribu tena hujifunza uwajibikaji na ustahimilivu. Mfumo huo wa uwajibikaji uliopangwa hukuza nidhamu ya ndani inayodumu hadi utu uzima. Hali hiyo ni tofauti na mtaa, ambao mara nyingi hutoa visingizio na kuhamisha lawama, nidhamu ya wazazi huwafundisha vijana kubeba matokeo ambayo ni chaguo lao na kuyatumia kujifunza.

Kutokana na hotuba hiyo ya Rais Samia kwa Wazee wa Mkoa wa Dar es Salaam, nilifanya uchunguzi katika moja ya vyuo vikuu ambavyo kwa historia vinaheshimika zaidi nchini Tanzania. Nilizungumza na mwenzangu ambaye kwa sasa ni mhadhiri kuhusu namna wanavyowafundisha nidhamu wanafunzi vijana wanaosoma chuo kikuu.

Nikabaini mambo kadhaa yanayosisitiza mtazamo wa Rais Samia kuhusu umuhimu wa wazazi kuwa karibu na watoto wao na kuwapa maarifa sahihi. Nikagundua haraka kwamba, matatizo yanayowakabili wahadhiri  chuoni hayajengwi ndani ya mazingira ya chuo, bali vijana hufika nayo yakiwa tayari yameundwa kwa miaka ya mafunzo ya nyumbani (utaratibu au ukosefu wa utaratibu) na tabia wanazokuwa nazo wanapokua.

Kimsingi, chuo kinaweza kuongoza, kushauri na kusahihisha. Hata hivyo, hakiwezi kujenga upya kitu ambacho hakikuwahi kujengwa yaani kujidhibiti, kuheshimu mipaka na uwezo wa kuvumilia uchovu wa akili bila kukimbilia kwenye runinga.

Nikajifunza pia kwamba, ninapojadili nidhamu katika mazingira ya kujifunzia katika maisha ya kila siku, kuna tabia ya kupunguza hadi mahudhurio, muda wa mwisho na tabia za darasani. Katika dalili hizi hasa katika bidhaa zinazopokewa na shule siku hizi, kuna vichocheo vikuu zaidi.

Hivi ni pamoja na ulalaji duni, upatikanaji usio na kikomo wa vifaa, vyakula visivyo na udhibiti, ulaji usiofaa, ushawishi, tabia dhaifu za kusoma, utekelezaji mdogo wa majukumu ya nyumbani pamoja na utamaduni wa kuridhika.

Kama nilivyobainisha awali, mambo hayo yanaonekana wazi katika mazingira ya kujifunzia. Kwa mfano, mtoto anayelelewa na simu chumbani sambamba na burudani kila anapohitaji, hufunza ubongo kutafuta msisimko wa mara kwa mara.

Je, tunatarajia akili ya mtoto kama huyo kukaa kwenye mihadhara, kufuatilia masomo kwa umakini, kuzingatia muda kuzingatia bila kuwekewa msingi wa mwongozo, au kuepuka vitendo visivyo vya kimaadili? Mara nyingi tunasikia wazazi wakisema maneno kama, “Tulijaribu kila kitu; ushauri, kukemea na hata mazungumzo ya kawaida,lakini hakuna kitu kinachofanya kazi.”

Kama mzazi ninajua ugumu uliopo, lakini pia unaonesha kutokuelewa kwamba, nidhamu ni mfumo na si kitendo cha kusema. Ufikiaji unapokosa kikomo na matokeo kutopatikana, maneno ama yawe ya upole au ya ukali, huwa kelele. Hoja za muda mrefu hufundisha kitu kimoja kwamba, nikisukuma sana, mpaka unaweza kubadilika. Kurudia kwa utulivu, pamoja na matokeo yasiyobadilika, hufundisha kitu bora zaidi kwamba, sheria ni muhimu.

Kama wazazi, hivi ndivyo tunavyoweza kubadilisha mawazo ya watoto wetu, ambao ni mustakabali wa taifa letu. Zama hizi za nyumba ya kisasa bila kujali kima cha mshahara, kiwango cha shughuli au elimu ama iwe katika sekta ya umma au ya binafsi zinakabiliwa na shinikizo jipya.

Zana za kufundishia zimeundwa kuvutia umakini, akiliunde hufanya njia za mkato zishawishi na kuvutia, na pia mitandao ya kijamii kama mtindo wa maisha, imeundwa kuchochea tamaa. Udhibiti haupaswi kuwa wa mara kwa mara, bali unapaswa kujengeka katika maisha ya kila siku.

Mwanzo wa vitendo ni seti ndogo ya vitu visivyoweza kujadiliwa: vifaa haviendi kulala, kazi ya nyumbani huja kabla ya burudani, milo hufanyika bila vifaa vya kufundishia, kulala kuna muda maalumu na harakati fulani za kimwili ni sehemu ya siku nyumbani.

Hizi si adhabu; ni hali za uendeshaji wa kujenga mawazo yenye afya. Hali kama hizo husaidia kulea mtoto au kijana hadi utu uzima anapoweza kutofautisha mema na mabaya. Kimsingi, katika kaya nyingi, nidhamu huporomoka kwa sababu upendo huoneshwa kupitia kiasi na wakati mwingine hali hiyo huimarishwa na wazee wanaosema: “Mwache mtoto afurahie.”

Wazee wanaweza kuwa nguvu ya kuleta utulivu endapo familia inakubaliana na kanuni moja kwamba, kamwe mapenzi hayapaswi kuvuka mipaka. Toa muda, weka umakini, andaa milo ya pamoja, hadithi na matembezi, badala ya muda wote kuwa wa kutazama skrini hata usiku sana au vitu visivyohitajika vya kila siku.

Shule, vyuo na vyuo vikuu pia vinalo jukumu. Wengi hulalamika kuhusu simu lakini huzivumilia; wengine huzidisha kazi kwa wanafunzi lakini hawafundishi tabia za kusoma na kuchanganua, usimamizi wa muda au usafi wa kidijiti.

Sera zilizo wazi kuhusu simu, kulindwa kwa muda wa kusoma, utaratibu mzuri wa kusoma na mwongozo kuhusu matumizi ya kimaadili ya mitandao ya kijamii kama msaidizi wa kujifunza badala ya nyenzo za udanganyifu utasaidia vijana kufika chuo kikuu wakiwa na tabia njema.

Si kwamba nadhihaki teknolojia na kile inachokileta, bali kufundisha watoto namna ya kuishi na teknolojia badala ya kumilikiwa nayo. Ombi kwa wazazi na walimu katika shule, vyuo na hata vyuo vikuu pia halina budi kuzingatiwa. Tatizo linapoanza mapema, hatupaswi kujifanya hatuna msaada.

Kwa mfano, mwelekeo wa mwaka wa kwanza unapaswa kuwa wa vitendo; namna ya kusoma, faida na hasara za matumizi ya mitandao ya kijamii, namna ya kuandika maelezo, kupanga kazi, kudhibiti visumbufu pamoja na suala la kujihusisha na makundi mbalimbali.

Nikiwa mhadhiri wa zamani wa chuo kikuu nchini Tanzania na kwingineko barani Ulaya, ninashauri jamii kuzingatia kuwa, tathmini na juhudi endelevu katika malezi ya vijana ni muhimu. Katika zama hizi za akiliunde na mitandao ya kijamii, ambapo kila mmoja ‘ni mwandishi wa habari’, utu na malezi sahihi ya watoto wetu yataimarika wakati wazazi tunatathmini mchakato unaofanya uelewa uonekane na uwe wa thamani na mgumu kupuuzwa.

Kimsingi nidhamu ni mradi wa pamoja katika malezi yote ya mtoto. Wazazi hutoa utaratibu, wazee hutoa uthabiti, shule hujenga tabia na vyuo vikuu huboresha ukomavu. Tabaka moja linaposhindwa, mengine yanayofuata hupambana. Kama nilimwelewa vizuri Rais Samia, nidhamu si mazungumzo ya kuhamasisha au ujuzi wa kuishi mitaani, bali ni mfumo wa tabia, mifano, na uwajibikaji unaoanzishwa mapema nyumbani.

Kama wazazi, tukiweza kujenga mfumo huu, vijana, viongozi wa baadaye ambao pia ni mali za taifa letu, watakuwa na nidhamu maishani, kimyakimya, kwa uthabiti na kwa ufanisi.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *