
Mara nyingi, mipango ya kimataifa kuhusu Palestina inapozinduliwa katika majukwaa kama Davos, huwasilishwa kwa lugha inayoashiria kuwa haina budi kutokea. Amani huonekana kama tatizo la kiufundi linaloweza kutatuliwa kupitia vikao, mifumo na makubaliano yanayosimamiwa kwa uangalifu.
“Bodi ya Amani” iliyozinduliwa katika Jukwaa la Uchumi Duniani ni jaribio jingine la kuleta msukumo katika mgogoro uliodumu kwa vizazi vingi.
Kwa Wapalestina, matukio kama haya si mageni. Ni taswira inayojirudia katika historia ndefu ya “masuluhisho” yaliyobuniwa kutoka nje — nyingi zikiwa na ahadi za dola, utulivu au ustawi, lakini matokeo yake yakiwa ni kuendelea kwa ukaliaji wa mabavu, mamlaka yaliyogawanyika, na kuungwa mkono dhuluma badala ya suluhu.
Kwa hiyo, tathmini yoyote makini ya Bodi ya Amani lazima ianze si tu kwa matarajio yake, bali kwa rekodi ya kisiasa inayoirithi.
Rais wa Marekani Donald Trump alizindua Bodi ya Amani kama chombo cha kutatua migogoro ya kimataifa, kwa gharama inayoripotiwa kufikia dola bilioni moja kwa wanachama wa kudumu.
Awali, bodi hiyo ilikusudiwa kusimamia ujenzi upya wa Gaza, lakini rasimu ya katiba yake haionyeshi kuweka majukumu yake katika ardhi ya Palestina pekee.
Afisa mmoja mwandamizi wa Ikulu ya White House amesema kuwa takribani nchi 35 — ikiwemo Uturuki — zimekubali kujiunga hadi sasa, kati ya mialiko karibu 50 iliyotumwa.
Maelezo haya ni muhimu. Yanaweka wazi kuwa Bodi ya Amani si chombo cha msaada kwa watu tu kinacholenga Gaza pekee, bali ni muundo mpya wa kisiasa wenye matarajio mapana, na uanachama wake unaoamuliwa na nguvu, na uwiano wa kisiasa.
Amani kwa namna gani?
Michakato ya amani hauegemei upande wowote. Huakisi mizani ya uwezo na vipaumbele vya kisiasa vilivyopo wakati wa kuanzishwa kwake, na mchakato huu hauna tofauti.
Muundo wa bodi unazidisha wasiwasi huu. Miongoni mwa nchi zinazodaiwa kushiriki ni Israel na baadhi ya washirika wakuu wa Marekani ambao ni Mashariki ya Kati, pamoja na serikali nyingine zilizo na uhusiano wa karibu wa kisiasa na Marekani.
Ushiriki wa Israel ni wenye uzito mkubwa. Waziri Mkuu Benjamin Netanyahu — ambaye serikali yake ilisimamia uharibifu mkubwa wa Gaza — yupo kama sehemu ya bodi inayodaiwa kuunda amani na ujenzi upya.
Hili halifanyi mpango huo kuwa batili moja kwa moja, lakini linaonyesha mvutano wa msingi uliokumba juhudi nyingi za kidiplomasia kuhusu Palestina: je, amani inachukuliwa kama mchakato unaojengwa juu ya uwajibikaji na haki, au kama jukwaa la kudumisha nguvu bila ya kuwepo kwa uwajibikaji?
Mvutano huu unaeleza kwa nini mashaka ya Wapalestina kuhusu mifumo mipya ya kidiplomasia si msimamo wa kiitikadi tu, bali ni uzoefu halisi wa kisiasa.
Kuanzia Oslo na kuendelea, mipango ya amani mara nyingi imeipa kipaumbele uratibu wa usalama, usimamizi wa uchumi na makubaliano ya mpito, huku ikiahirisha au kupunguza masuala ya msingi ya mgogoro: ukaliaji wa mabavu, mamlaka kamili, mipaka, wakimbizi na usawa mbele ya sheria.
Matokeo hayakuwa amani, bali kuongezeka kwa nguvu iliyoimarisha ukaliaji wa Israel na kudhoofisha matumaini ya dola huru ya Palestina.
Hatari ya Bodi ya Amani si tu kwamba inaweza kufeli. Hatari kubwa ni kwamba inaweza “kufanikiwa” kwa kuubadili mgogoro kwa namna inayopunguza matarajio.
Ujenzi upya bila mamlaka, misaada bila haki, na utulivu bila haki ya kijamii ni matokeo yaliyozoeleka ya michakato ya zamani.
Bodi itakayochukulia Gaza kama changamoto ya kiufundi ya ujenzi pekee, badala ya kuwa sehemu ya mapambano mapana ya kisiasa ya kujitawala, iko katika hatari ya kurudia makosa hayo.
Maono ya Trump ya Gaza iliyojengwa upya, yenye majengo ya kifahari na fukwe zilizojaa mitende, ni kejeli kwa mateso waliyopitia Wapalestina wa Gaza katika miaka miwili iliyopita, ardhi yao ya nyumbani ikigeuzwa kuwa mandhari ya kutisha na maeneo ya vita ya Israel.
Hata hivyo, itakuwa si sahihi — na si busara kimkakati — kuipuuza Bodi ya Amani kama jambo lisilo na maana.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Uturuki, Hakan Fidan, aliweka suala hili katika muktadha sahihi alipoiita Bodi ya Amani “fursa ya kihistoria” ya kumaliza mateso ya muda mrefu ya Wapalestina.
Mtazamo wake unaakisi matumaini ya Rais Recep Tayyip Erdogan — mmoja wa watetezi wakubwa wa suala la Palestina — kwamba mipango yote inayolenga kuleta amani Gaza ni ya muhimu.