Idadi ya wageni walioajiriwa nchini Japani ilifikia kiwango cha juu zaidi mwaka jana, ikizidi milioni 2.5 kwa mara ya kwanza na kuangazia uhaba wa wafanyakazi nchini humo.

Wizara ya Afya, Kazi na Ustawi wa Jamii ilisema kufikia mwisho wa mwezi Oktoba, raia wa kigeni 2,571,037 walikuwa wameajiriwa nchini Japani.

Idadi hiyo ni ya juu zaidi tangu wizara hiyo ilipoanza kuwataka waajiri kuripoti wafanyakazi wao wa kigeni mwaka 2007.

Idadi hiyo iliongezeka kwa 268,450 kutoka mwaka 2024.

Wizara pia ilisema kiwango cha ukuaji wa mwaka hadi mwaka kilikuwa asilimia 11.7, kikizidi alama ya asilimia 10 kwa mwaka wa tatu mfululizo.

Wafanyakazi wa Vietnam walichangia sehemu kubwa zaidi ya wafanyakazi kwa takribani 606,000, wakifuatiwa na Wachina kwa takribani 432,000, wale kutoka Ufilipino kwa takribani 261,000, Wanepali kwa takribani 236,000 na Waindonesia kwa takribani 228,000.

Ikiakisi uhaba mkubwa wa wafanyakazi katika baadhi ya viwanda, idadi ya wafanyakazi wa kigeni katika sekta ya matibabu na ustawi iliongezeka kwa asilimia 25.6 kutoka mwaka 2024, ongezeko kubwa zaidi miongoni mwa sekta. Idadi hiyo iliongezeka kwa asilimia 17.1 katika sekta ya malazi, kula na kunywa, ikifuatiwa na ongezeko la asilimia 16.1 katika sekta ya ujenzi.

Wizara ya kazi ilisema wafanyakazi wa kigeni wamechangia ongezeko la jumla katika miaka ya hivi karibuni. Wizara hiyo iliongeza kuwa inatumai kuendelea kuboresha mazingira ya kazi ili wafanyakazi wa kigeni waweze kutumia vipaji vyao kikamilifu.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *