
Dar es Salaam. Yanga imeshindwa kutambiana na Al Ahly baada ya kulazimishwa sare ya bao 1-1 katika mchezo wa nne wa hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika.
Matokeo hayo yamezidi kuongeza ugumu katika kundi lao B ambalo kwa sasa timu zote nne zilizopo hapo kila moja ina uwezekano wa kufuzu robo fainali.
Yanga imekuwa ya kwanza kupata bao katika mchezo huo kupitia kwa Ibrahim Abdullah ‘Bacca’ aliyefunga katika dakika ya 45 akimalizia mpira uliookolewa vibaya na Aliou Dieng.
Muda mfupi baada ya kuingia bao hilo, Mwamuzi Antoine Effa Essouma kutoka Cameroon alipuliza filimbi ya kuashiria muda wa mapumziko.
Kipindi cha pili kilianza kwa Al Ahly kulishambulia mfululizo lango la Yanga na juhudi zao zilizaa matunda katika dakika ya 60 walipopata bao la kusawazisha kupitia wa Dieng aliyeunganisha vyema pasi ya Mahmoud Hassan ‘Trezeguet’.
Baada ya Al Ahly kusawazisha, timu hizo zilianza kushambuliana kwa zamu kila moja ikionekana kujaribu kusaka bao la pili lakini safu zao za ulinzi zilikuwa imara kuokoa hatari ambazo zilielekezwa katika milango yao.
Katika kipindi hicho cha pili, Al Ahly ilifanya mabadiliko ya kuwatoa Marwan Attia, Mohamed Taher, Ahmed Zizo na Yasser Ibrahim ambao nafasi zao zilichukuliwa na Achraf Bencharki, Mohamed Ben Romdhane, Ahmed Eid na Ahmed Ramadan.
Yanga ilifanya mabadiliko ya kuwatoa Chadrack Boka, Depu na Allan Okello na kuwaingiza Mohamed Hussein, Prince Dube na Israel Mwenda.
Hata hivyo mabadiliko hayo hayakuweza kubadilisha ubao wa matokeo na hadi filimbi ya kumaliza mchezo inapulizwa, timu hizo ziligawana pointi.
Sare hiyo imefanya Al Ahly izidi kujichimbia kileleni mwa msimamo wa kundi B la Ligi ya Mabingwa Afrika msimu huu ikiwa na pointi nane huku Yanga ikifikisha pointi tano.
Baada ya mechi hiyo, kibarua kinachofuata kwa Yanga hivi sasa ni mchezo wa ugenini dhidi ya FAR Rabat ya Morocco ambao umepangwa kuchezwa Jumamosi ijayo, Januari 7.