Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres, amezishauri nchi wanachama kulipa michango yao, akionya kwamba Umoja wa Mataifa unakabiliwa na hatari ya mdororo wa kifedha kutokana na kiasi kikubwa cha madeni.

Katika barua yake aliyoituma kwa nchi wanachama kufikia Jumatano Januari 28, Guterres alisema Umoja wa Mataifa ulimaliza mwaka 2025 ukiwa na madeni yasiyolipwa kiasi cha dola bilioni 1.568, ikiwa ni zaidi ya mara mbili ya kiasi cha mwaka uliotangulia.

Alisema fedha taslimu za bajeti ya kawaida ya Umoja wa Mataifa zinaweza kuisha kabisa ifikapo mwezi Julai. Alitoa wito kwa nchi zote wanachama kutimiza wajibu wao wa kulipa kikamilifu na kwa wakati.

Mdororo huo wa kifedha kwa kiasi kikubwa unahusishwa na kiasi ambacho hakijalipwa kutoka Marekani. Ikiwa inachangia kwa asilimia 22, Marekani inachangia kiasi kikubwa zaidi cha michango inayohitajika kufadhili bajeti ya Umoja wa Mataifa.

Mchango wa kila nchi huamuliwa kulingana na uwezo wake wa kiuchumi pamoja na uwezo wa kulipa.

Utawala wa Rais wa Marekani, Donald Trump, umekuwa ukiukosoa Umoja wa Mataifa. Chini ya shinikizo kutoka kwa Marekani, chombo hicho cha dunia kimelazimika kufanya mageuzi, ikiwa ni pamoja na kuhamisha wafanyakazi na kupanga upya vitengo vyake.

Guterres alisema katika taarifa yake iliyotolewa Januari 8 kwamba michango hiyo ni “wajibu wa kisheria chini ya Mkataba wa Umoja wa Mataifa kwa Nchi zote Wanachama, ikiwa ni pamoja na Marekani.”

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *