Waziri Mkuu wa Ethiopia, Abiy Ahmed, amesema kuwa nchi hiyo haikupokea “hata senti moja” kutoka kwa serikali yoyote ya kigeni kwa ajili ya kufadhili ujenzi wa Bwawa Kuu la Renaissance la Ethiopia (GERD), akikanusha madai ya Rais wa Marekani, Donald Trump, kwamba Marekani imefadhili mradi huo.

Akihutubia Bunge, Abiy amesema bwawa hilo limefadhiliwa kikamilifu kwa rasilimali za Ethiopia pekee, ikiwemo kampeni za miaka kadhaa za kukusanya michango ya umma.

Bwawa hilo, lililojengwa kwenye Mto Nile karibu na mpaka wa Sudan, ni mradi mkubwa zaidi wa umeme wa maji barani Afrika na limekuwa chanzo cha mvutano na Misri na Sudan, ambazo zimekuwa zikihofia athari zake kwenye mtiririko wa maji.

Abiy pia amesema kuwa Ethiopia ipo kwenye hatua za mwisho za mradi mwingine mkubwa wa umeme wa maji kwenye Mto Omo, wenye uwezo wa megawati 2,200 na uzalishaji wa mwaka wa takribani gigawati-saa 6,460.

Akizungumza katika Ikulu ya White House mwishoni mwa Januari, Trump alihoji kwa nini Marekani imefadhili bwawa hilo, madai ambayo maafisa wa Ethiopia wameshasema mara kadhaa kuwa si ya kweli.

Katika barua yake kwa Rais wa Misri, Abdel Fattah el-Sisi, Trump pia alipendekeza mazungumzo mapya kuhusu bwawa hilo.

Ripoti zinaeleza kuwa barua hiyo, iliyosambazwa pia kwa viongozi wa kikanda, ilitoa pendekezo la kuanza upya juhudi za upatanishi kwa lengo la kutatua mizozo ya muda mrefu kuhusu mgawanyo wa maji ya Nile.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *