
Kansela wa Ujerumani Friedrich Merz, leo anaanza ziara yake ya kwanza katika eneo muhimu lenye utajiri na la kimkakati la Ghuba. Kituo cha kwanza kitakuwa Saudi Arabia na kisha kufuatiwa na Qatar na Umoja wa Falme za Kiarabu. Merz analenga kuimarisha ushirikiano na mataifa yanayosafirisha mafuta na gesi, huku ushirikiano huo ukitarajiwa kujikita haswa katika sekta ya nishati.
Mazungumzo yake pia yatagusia mikataba ya silaha. Serikali zilizopita zilikuwa makini katika suala la mauzo ya silaha kwa nchi hizo tatu kutokana na masuala ya haki za binadamu na ushiriki wao katika migogoro ya kikanda. Ajenda nyingine itakuwa ni kuongezeka kwa mvutano kati ya Iran na Marekani na hofu ya kuzuka kwa vita mpya, mnamo wakati Rais Donald Trump akiendelea kuutishia uongozi wa Tehran kwa mashambulizi ya kijeshi.