Marekani, Iran zaanza kuzungumza kwa kutishianaMarekani, Iran zaanza kuzungumza kwa kutishiana

Mazungumzo ya ngazi ya juu kati ya Iran na Marekani yameanza rasmi Ijumaa nchini Oman, yakilenga kupunguza mvutano juu ya mpango wa nyuklia wa Tehran na kuzuia mzozo mpya katika ukanda wa Mashariki ya Kati.

Kwa mujibu wa vyombo vya habari vya serikali ya Iran, mazungumzo hayo yanafanyika katika mji mkuu wa Muscat, chini ya usimamizi wa Oman kama mpatanishi wa muda mrefu kati ya mataifa hayo mawili hasimu.

Hii ni duru ya kwanza ya mazungumzo tangu Marekani ijiunge na mashambulizi ya Israel dhidi ya Iran mwezi Juni mwaka jana, wakati wa vita vya siku 12 vilivyoharibu miundombinu kadhaa ya kijeshi na nyuklia ya Iran.

Wakati huo, Marekani ilishambulia baadhi ya vituo vya nyuklia vya Iran, ikisema ilikuwa inalenga kuzuia Tehran kusonga mbele na mpango wake wa nyuklia.

Tangu wakati huo, mvutano umeendelea kuongezeka, huku pande zote zikitoa matamshi makali na kuonyesha utayari wa kuchukua hatua kali iwapo diplomasia itashindwa.

Oman Maskat 2026 | Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran Abbas Araghchi akiwa katika mazungumzo kuhusu mpango wa nyuklia wa Iran
Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran Abbas Araghchi akiwasili kukutana na mwenzake wa Oman kabla ya mazungumzo yanayotangazwa kwa udhamini wa Oman na Marekani.Picha: Iranian Foreign Ministry/ZUMA/IMAGO

Oman yarejesha jukumu la upatanishi

Ujumbe wa Iran unaongozwa na Waziri wa Mambo ya Nje Abbas Araghchi, ambaye amesema Tehran inaingia kwenye mazungumzo kwa “macho wazi” na kumbukumbu thabiti ya yaliyotokea mwaka uliopita.

Kwa upande wa Marekani, ujumbe unaongozwa na mjumbe maalum wa Mashariki ya Kati, Steve Witkoff, mshirika wa karibu wa Rais Donald Trump.

Araghchi amesema Iran iko tayari kwa mazungumzo ya dhati lakini haitakubali masharti yanayokiuka haki na mamlaka yake ya kitaifa.

Amesisitiza kuwa makubaliano yoyote lazima yajengwe juu ya heshima ya pande zote, usawa na maslahi ya pamoja ili yaweze kudumu.

Iran pia imesema iko tayari kujilinda dhidi ya kile ilichokiita “madai ya kupita kiasi” kutoka Washington.

Trump atoa onyo kali

Kabla ya mazungumzo kuanza, Rais Donald Trump alitoa onyo kali kwa Kiongozi Mkuu wa Iran, Ayatollah Ali Khamenei, akisema anapaswa kuwa na wasiwasi mkubwa.

Trump alisema Iran ilikuwa inafikiria kuanzisha kituo kipya cha nyuklia katika sehemu nyingine ya nchi, na akaonya kwamba Marekani itachukua hatua kali iwapo hilo litafanyika.

Aidha, Trump amesisitiza kuwa hataki kuona Iran ikiwa na uwezo wowote wa nyuklia, akieleza wazi kuwa lengo lake ni “kutokuwepo kabisa kwa uwezo wa nyuklia.”

Ikulu ya White House imesema rais ana chaguzi nyingi mezani mbali na diplomasia, akitumia mamlaka yake kama Amiri Jeshi Mkuu wa jeshi lenye nguvu zaidi duniani.

Marekani pia imetuma kundi la meli za kivita, likiwemo lile linaloongozwa na manowari ya USS Abraham Lincoln, katika eneo la Ghuba, hatua inayoongeza presha kwa Tehran.

USA Washington D.C. 2025 | Donald Trump akifuatilia mashambulizi dhidi ya vituo vya nyuklia vya Iran katika Situation Room
Rais Donald Trump alitoa onyo kali kwa Kiongozi Mkuu wa Iran, Ayatollah Ali Khamenei, akisema anapaswa kuwa na wasiwasi mkubwa.Picha: THE WHITE HOUSE/UPI Photo/Newscom/picture alliance

Tofauti za ajenda zatishia mazungumzo

Wakati Iran ikisisitiza kuwa mazungumzo yajikite tu kwenye mpango wake wa nyuklia, Marekani inataka pia kujadili makombora ya balistiki ya Tehran na uungwaji mkono wake kwa makundi yenye silaha katika kanda.

Washington pia imeeleza wasiwasi kuhusu hali ya haki za binadamu nchini Iran, hasa baada ya ukandamizaji wa maandamano makubwa ya kitaifa mwezi uliopita.

Ripoti za makundi ya haki za binadamu zinasema maelfu waliuawa au kukamatwa wakati wa operesheni za usalama zilizofuata maandamano hayo.

Kwa upande mwingine, Iran imekuwa ikisisitiza kuwa mpango wake wa nyuklia ni wa matumizi ya amani tu na kwamba haina nia ya kutengeneza silaha za nyuklia.

Hata hivyo, mataifa ya Magharibi yanaamini kuwa Tehran inaweza kuwa inatafuta uwezo wa kutengeneza silaha, madai ambayo Iran imekanusha mara kwa mara.

Trump aitoa Marekani makubaliano ya nyuklia ya Iran

To view this video please enable JavaScript, and consider upgrading to a web browser that supports HTML5 video

Hofu ya mzozo mpana zaidi

Iran inaripotiwa kuwa tayari kuonyesha unyumbufu katika suala la urutubishaji wa urani, ikiwa ni pamoja na uwezekano wa kupunguza kiwango au kukabidhi akiba fulani ya urani iliyorutubishwa kwa kiwango cha juu.

Lakini Tehran inasisitiza kuwa haki yake ya kurutubisha urani haiwezi kujadiliwa na inataka kuondolewa kwa vikwazo vya kiuchumi vilivyowekwa tena tangu mwaka 2018.

Mataifa ya Ghuba ya Uajemi yanafuatilia kwa karibu mazungumzo haya, yakihofia kuwa kushindwa kwa diplomasia kunaweza kusababisha mashambulizi ya kijeshi na kuutumbukiza ukanda mzima kwenye vita.

Viongozi wa kimataifa wamehimiza pande zote kuonyesha unyumbufu na kuepuka hatua zitakazoongeza mvutano.

Kwa sasa, macho ya dunia yameelekezwa Muscat, ambako mustakabali wa makubaliano mapya ya nyuklia unaweza kuamuliwa katika siku zijazo.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *