Maafisa waandamizi kutoka Ukraine, Urusi na Marekani wamekutana kwa ajili ya awamu nyingine ya mazungumzo ya kukomesha mapigano. Wamesema walibadilishana wafungwa 157 kutoka Ukraine na 157 kutoka Urusi baada ya mkutano huo.

Rais wa Ukraine Volodymyr Zelenskyy alisema kwenye mitandao ya kijamii Februari 5 kwamba mateka hao walijumuisha maafisa kutoka Vikosi vya Kijeshi, Kikosi cha Walinzi wa Taifa na Huduma ya Walinzi wa Mpakani ya Taifa pamoja na raia. Aliongeza kuwa wengi wao wameshikiliwa tangu mwaka 2022.

Wizara ya Ulinzi ya Urusi ilithibitisha kuachiliwa huru kwa watu wake na kusema watapata matibabu na kurejeshwa katika maisha ya kawaida.

Mazungumzo ya amani yaliyofanyika katika mji mkuu wa Umoja wa Falme za Kiarabu, Abu Dhabi Februari 4 na 5, yalijumuisha Mnadhimu Mkuu wa Ukraine, Kyrylo Budanov, na Igor Kostyukov ambaye ni mkuu wa idara ya ujasusi ya kijeshi ya Urusi. Mjumbe maalum wa Marekani Steve Witkoff aliongoza upande wa Marekani.

Witkoff alisema kwenye mitandao ya kijamii kwamba kazi zaidi inahitaji kufanywa, lakini anatarajia hatua zaidi kupigwa “katika wiki zijazo.”

Bado haijulikani wazi ikiwa hatua ilipigwa kuhusu masuala ya eneo na hakikisho la usalama kwa Ukraine.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *