WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Profesa Riziki Shemdoe ameridhishwa na hatua iliyofikiwa ya maandalizi ya ufunguzi Soko Kuu la Kariakoo, Dar es Salaam.
Profesa Shemdoe alieleza kuridhishwa na maandalizi hayo jana alipotembelea soko hilo ili kujiridhisha na maandalizi ya hafla ya ufunguzi wa soko hilo litakalofunguliwa na Rais Samia Suluhu Hassan leo.
Aidha, alimshukuru Rais Samia kwa uwekezaji uliofanyika katika soko hilo lililoungua mwaka 2021 ambapo limefanyiwa ukarabati na kujengwa soko lingine jipya lenye ghorofa sita katika eneo hilo.
“Ninamshukuru Rais (Samia) kwa Shilingi bilioni 28 aliyoridhia itumike kwa ajili ya ukarabati na ujenzi huu, hii ni hatua kubwa sana ambayo tunapaswa kujivunia,” alifafanua Profesa Shemdoe.
Soko Kuu la Kariakoo liliungua Julai 10, 2021 na Rais Samia alipotembelea soko hilo kuwapa pole wafanyabiashara waliopatwa na kadhia hiyo, aliahidi kuwa atafanya ukarabati na kuliboresha zaidi, ahadi ambayo ameitekeleza kwa vitendo. Profesa Shemdoe aliwasihi wananchi na wafanyabiashara wa Dar es Salaam kujitokeza kwa wingi katika uzinduzi wa soko hilo huku akiwapongeza viongozi wa Mkoa wa Dar es Salaam pamoja na uongozi wa Shirika la Masoko ya Kariakoo kwa namna walivyoshirikiana na kufanikisha maandalizi hayo kwa kiwango cha juu.
