MSANII nyota wa muziki wa Bongo Fleva na Mkurugenzi Mtendaji wa Wasafi Media, Diamond Platnumz anajiandaa kuachia wimbo wake mpya wa kimahaba uitwao ‘Natulizana’ ikiwa ni maalum kwa msimu wa Valentine. Hata hivyo, mbali na mashabiki kusubiri kwa hamu wimbo huo , gumzo kubwa limeibuka kuhusu saa ya kifahari inayoonekana kwenye video ya wimbo huo yenye thamani ya Sh1.2 bilioni.
Katika kikao cha maandalizi ya video hiyo pamoja na timu yake ya uzalishaji akiwemo kaka yake Romy Jons.“Kuna kidonga watch kimoja cha 1.2B hapo kimeoneshwa,” aliandika Diamond kupitia ukurasa wake wa Instagram huku akiitambulisha timu ya watayarishaji wa video hiyo, jambo lililozua mjadala mkali mitandaoni.
Diamond si mgeni katika kuonesha maisha ya kifahari. Mwaka jana alionekana akiwa amevalia mavazi ya wabunifu wa kimataifa yenye thamani ya dola 265,000. Katika mahojiano ya mwaka 2016, msanii huyo alikadiria utajiri wake kufikia dola milioni 4, huku mwaka 2018 akihamia katika jumba lake la kifahari lililopo Mbezi Beach, Dar es Salaam.
Mbali na mavazi, Diamond anafahamika kwa kumiliki magari ya kifahari, yakiwemo Rolls-Royce Cullinan ya mwaka 2021 na Cadillac Escalade zilizoboreshwa maalum. Aidha, ripoti mbalimbali zimekuwa zikieleza uwezo wake wa kutumia usafiri wa hadhi ya juu ikiwemo ndege binafsi. SOMA: Ciara,Diamond Platnumz wazindua ‘Low’”
Pia anatajwa kumiliki vito vya thamani, ikiwemo saa aina ya Richard Mille RM 011 na grillz za meno zilizopambwa kwa almasi. Wakati mashabiki wakisubiri kuiona video ya ‘Natulizana’, ni wazi kuwa mbali na muziki, mitindo na maisha ya kifahari ya Diamond Platnumz yataendelea kuwa gumzo ndani na nje ya Tanzania.
