MALAWI;  WAFANYABIASHARA wadogo  watanufaika na  Mfumo Rahisi wa Kurahisisha na Kuimarisha biashara  (STR) zinazofanyika katika mipaka ya Tanzania na Malawi, hususan mpaka mkubwa wa Kasumulo na Songwe.

Makubalino hayo ni moja ya maono ya Rais wa Tanzania, Dk Samia Suluhu Hassan, ambaye mara zote anapenda masuala ya biashara yanufainishe vijana na wanawake ambao hufanya shughuli za biashara kila siku.

Hayo yamebainishwa na Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga wakati wa hafla ya kusaini mkataba wa makubaliano baina ya nchi ya Tanzania na Malawi Februari 16,2026, jijini Lilongwe, Malawi.

Waziri Kapinga amesema mkataba wa makubaliano hayo ni muhimu kwa wafanyabiashara hususani vijana na wanawake, kwani utarahisisha ufanyaji biashara na kupunguza urasimu,  ambao ulikuwepo awali pamoja na kuwa na utaratibu wa kupata huduma kwa  haraka ikiwemo ujazaji fomu ya uasili papo hapo na kuendelea na biashara kwa upande wa pili.

Amesema mkataba huo unajunuisha mfumo maalumu wa biashara unaolenga kurahisisha taratibu za forodha na kupunguza vikwazo visivyo vya kikodi (NTBs) kwa wafanyabiashara wadogo wanaofanya biashara za kuvuka mipaka ya Tanzania na Malawi (Cross Border Trade).

Aidha, amebainisha kuwa mkataba huo uliotiwa saini unahusisha Mfumo STR, ambao utaruhusu wafanyabiashara wadogo kusafirisha bidhaa zilizoainishwa kwenye mkataba huo kwa kutumia nyaraka chache, fomu rahisi za kiforodha na za uasili wabidhaa kwa kuzingatia kiwango maalumu cha thamani ya bidhaa kilichowekwa katika mkataba bila kupitia taratibu ndefu za kawaida za forodha.

Waziri Kapinga pia amesema kusainiwa kwa Mkataba wa STR kati ya Tanzania na Malawi kutakuza biashara halali mpakani,  ambapo Wwfanyabiashara wadogo watahamasika kufanya biashara kwa kufuata taratibu rasmi badala ya njia zisizo rasmi, kupunguza gharama za biashara, kuongeza mapato ya serikali na kuimarisha uhusiano wa kiuchumi kati ya Tanzania na Malawi.

Amebainisha kuwa utaratibu huo utawahusisha wafanyabiashara wenye mitaji isiyozidi dola za Kimarekeni 2000.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *