Adhabu ya kifo, kifungo cha maisha, au msamaha dhidi ya uwezekano wowote? Rais wa zamani wa Korea Kusini Yoon Suk Yeol atajua hatima yake leo Alhamisi katika kesi kuu inayohusiana na sheria ya kijeshi, ambayo alitangaza mnamo mwezi Desemba 2024 katika mapinduzi ya ghafla na mafupi.

Imechapishwa:

Dakika 3 Wakati wa kusoma

Matangazo ya kibiashara

Kwa kuwa hatia yake inachukuliwa kwa mashaka, majaji katika Mahakama ya Wilaya ya Kati ya Seoul wanatarajiwa kuchagua kati ya adhabu ya kifo, iliyoombwa na upande wa mashtaka, na kifungo cha maisha jela, njia mbadala pekee iliyotolewa na sheria kwa uhalifu wa uasi.

Hakuna adhabu ya kifo iliyotekelezwa nchini Korea Kusini tangu mwaka 1997. Lakini wafungwa kadhaa wanaendelea kusubiri adhabu yao ya kifo iweze kutekelezwa.

Jioni ya Desemba 3, 2024, kiongozi huyo wa zamani wa kihafidhina, akitaja tishio la “vikosi vinavyopinga serikali,” bila kutarajia alitangaza sheria ya kijeshi kwenye televisheni, huku jeshi likipelekwa kuzingira Bunge na kulinyamazisha.

Kusimamishwa kwa utawala wa kiraia hatimaye kulidumu kwa saa sita pekee. Usiku wa manane, baadhi ya wabunge, kwa kupanda uzio wa pembezoni, waliweza kuingia ndani ya jengo la Bunge kwa wingi wa kutosha kuzuia mipango ya Yoon Suk Yeol.

Jaribio lake lilifufua kumbukumbu zenye uchungu za udikteta katika jamii ambayo ilikuwa imezoea utulivu wa kidemokrasia, lilitikisa masoko, lilishangaza ulimwengu, na kusababisha mgogoro mkubwa wa kisiasa wa ndani.

Nchi ilishuhudia matukio kadhaa: Bunge kumtimua kwa muda Yoon  Bunge, kukamatwa kwake—katika jaribio la pili la mamlaka—kuondolewa kwenye wadhifa wake mwezi Aprili, na kisha ushindi wa mpinzani wake, Lee Jae Myung, katika uchaguzi wa rais wa mapema mwezi Juni.

Wakorea Kusini, ambao waliandamana kwa wingi kumtetea na kumpinga Yoon Suk Yeol kwa miezi kadhaa baada ya usiku huo, wanatarajiwa kufikia mamilioni kufuata hukumu hiyo, ambayo inatarajiwa kutolewa kuanzia saa 9:00 alasiri saa za Korea Kusini (saa 1:00 asubuhi saa za Ufaransa).

Maelfu ya wafuasi wake wamekusanyika nje ya mahakama, wakitaka mashtaka hayo yafutwe.

Shangwe zilizuka wakati basi la gereza la bluu, linalodhaniwa kuwa lilikuwa likimsafirisha kiongozi wao, lilipofika.

Akiwa kizuizini, Yoon, mwenye umri wa miaka 65, anakabiliwa na kesi kadhaa za jinai.

Katika kesi hiyo itakayoamuliwa leo Alhamisi, waendesha mashtaka wanamshtaki kwa kuongoza “uasi” uliosababishwa na “kiu ya madaraka.”

Kulingana na wakili na mchambuzi wa masuala ya siasa Yoo Jung-hoon, kifungo cha maisha ndio matokeo yanayowezekana zaidi.

“Mara chache, jaji anaweza kutumia kile kinachojulikana kisheria kama ‘kupunguza upendeleo kwa hiari,’ kuweka hukumu nyepesi kuliko kiwango cha chini kilichowekwa na sheria ikiwa wanaamini ni sahihi,” ameongeza.

“Lakini Yoon hajakiri hatia wala kuonyesha majuto, kwa hivyo itakuwa vigumu kwa baraza la majaji kutoa hukumu nyepesi kuliko kifungo cha maisha,” Yoo ameliambia shirika la habari la AFP.

Rais huyo wa zamani amekuwa akikana makosa yoyote, akidai kwamba alichukua hatua ya “kuhifadhi uhuru” na kurejesha utaratibu wa kikatiba dhidi ya kile alichokiita “udikteta wa kisheria” wa upinzani, ambao ulitawala Bunge na kuzuia miradi yake.

Tayari amehukumiwa kifungo cha miaka mitano jela kwa makosa madogo madogo yanayohusiana na mapinduzi yake. Washirika wa zamani, ambao walikuwa madarakani wakati wa uamuzi wake wa kushangaza, pia wamehukumiwa kifungo au wanasubiri kesi.

Miongoni mwao ni Waziri Mkuu wa zamani Han Duck-soo, ambaye alihukumiwa kifungo cha miaka 23 jela (ikilinganishwa na miaka 15 iiliyoombwa na upande wa mashtaka) mwishoni mwa mwezi Januari, na Waziri wa Mambo ya Ndani wa wakati huo, Lee Sang-min, ambaye alihukumiwa kifungo cha miaka saba jela wiki iliyopita kwa majukumu yao katika kashfa hiyo.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *