KAMISHNA wa Uhifadhi wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Prof Dos Santos Silayo, amewataka viongozi na makamanda wa vituo vya wakala huo kubadili mtazamo wa uongozi kwa kusikiliza wananchi, kuwaelewa vijana wa ajira mpya na kusimamia migogoro ya rasilimali kwa busara, akisisitiza kuwa ofisi za umma hazina kisingizio cha kuchelewesha majibu kwa wananchi.

Prof. Silayo amesea hayo wakati akizungumza leo Februari 19, 2026 katika siku ya pili ya Mkutano wa Nne wa Viongozi na Makamanda wa Vituo vya TFS unaoendelea mjini Morogoro.

Amesema mabadiliko ya kijamii na kimazingira yanailazimu TFS kuwa na fikra pana zaidi na mbinu mpya za uongozi na utatuzi wa changamoto.

“Serikali imeweka mwelekeo wa kuwasikiliza wananchi. Hivyo, kila kiongozi wa TFS kwa nafasi yake anapaswa kuwa tayari kusikiliza, kujibu na kutatua changamoto zinazoletwa mezani. Ofisi ni ya Serikali; haijalishi ulikuwepo au hukuwepo wakati tatizo linaanza,” amesisitiza.

Prof Silayo amesema TFS inapaswa kuendana na kasi ya mabadiliko ya kijamii yanayoathiri mitazamo ya vijana wanaoajiriwa sasa, akibainisha kuwa kizazi kipya kina matarajio tofauti kuhusu mazingira ya kazi.

“Leo kijana anaajiriwa akiwa tayari na matarajio maalum. Hatuwezi kuwachukulia kama wasikilizaji tu; tunapaswa kuwaheshimu, kuwaongoza na kuwajengea motisha,” amesema, akihimiza viongozi wa vituo kuwa tayari kupokea mawazo mapya na kuimarisha mazingira ya kazi yanayozingatia utu na heshima.

Akizungumzia athari za mabadiliko ya tabianchi na shinikizo la kijamii, Prof Silayo amesema ongezeko la mahitaji ya rasilimali linaweza kuchochea migogoro kati ya wananchi na hifadhi, hivyo akawataka viongozi kusimamia hali hiyo kwa weledi.

Ametoa mfano wa baadhi ya wananchi wanaochoma misitu kwa lengo la kujikinga dhidi ya wanyamapori waharibifu, akisema hatua hizo ni matokeo ya “mikakati ya kuishi” inayotokana na msongo wa kimazingira.

“Hatuwezi kupuuza dalili hizi. Ni lazima tuwafikie wananchi, tuwasikilize na tushirikiane nao kabla madhara hayajawa makubwa,” amesema.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *