Jumla ya Wakenya 1,000 wameajiriwa kupigania Urusi, kulingana na ripoti ya ujasusi ya Kenya inayoelezea mtandao wa maafisa wahalifu wanaodaiwa kushirikiana na makundi ya biashara haramu ya binadamu.

Imechapishwa:

Dakika 3 Wakati wa kusoma

Na: RFI na mashirika mengine

Matangazo ya kibiashara

Ripoti hiyo, iliyowasilishwa bungeni siku ya Jumatano na Idara ya Ujasusi ya Kenya (NIS), inasema Wakenya 89 walikuwa mstari wa mbele katika vita kati ya Urusi na Ukraine kufikia mwezi Februari mwaka huu.

Angalau Mkenya mmoja amefariki, huku wengine kadhaa wakirejea nyumbani wakiwa wamejeruhiwa au wamepatwa na mshtuko, ripoti hiyo inaongezwa.

Serikali ya Kenya, ambayo hapo awali ilikadiria kwamba takriban raia wake 200 waliajiriwa kupigania Urusi, inataka Moscow kuzuia kuajiri wanajeshi wa Kenya.

Akiwasilisha ripoti hiyo kwa wabunge, kiongozi wa walio wengi bungeni Kimani Ichung’wah, alifichua kile alichokiita mtandao “unaosumbua sana” wa maafisa wa serikali wahalifu wanaodaiwa kushirikiana na makundi ya biashara haramu ya binadamu ili kuwaajiri na kuwasafirisha Wakenya kupigana vita kati ya Urusi na Ukraine.

Idara ya ujasusi imeelezea kwa undani jinsi mashirika ya kuajiri yanavyodaiwa kushirikiana na wafanyakazi wa uwanja wa ndege wa Kenya, maafisa wa uhamiaji, maafisa katika Kurugenzi ya Upelelezi wa Jinai (DCI), maafisa wa kupambana na dawa za kulevya na maafisa wa Mamlaka ya Kitaifa ya Ajira ili kurahisisha usafiri wa waajiriwa.

Ichung’wah amedai kwamba mashirika hayo pia yamekuwa yakishirikiana na wafanyakazi katika ubalozi wa Urusi jijini Nairobi na ubalozi wa Kenya jijini Moscow ili kuwasaidia waajiriwa kupata visa vya Urusi.

Urusi hapo awali ilikana kuhusika kokote katika kuwaajiri Wakenya kupigana nchini Ukraine.

Ichung’wah alisema kwamba balozi wa Kenya huko Moscow “lazima aweze kuwatambua maafisa wa ubalozi ambao huenda walikula njama na wahalifu hawa. Ubalozi wetu lazima uwe bila lawama. Lazima uwe mahali ambapo Wakenya wanaweza kupata kimbilio, si mahali pa kuwatumia kwa maslahi ya watu binafsi.”

“Ofisi za serikali hazipaswi kutumika kwa shughuli za uhalifu,” aliongeza.

Ripoti hiyo haikusema kilichowapata wengi wa waajiriwa lakini imesema kwamba pamoja na wale walio mstari wa mbele, wengine 35 wamepelekwa kwenye kambi za kijeshi nchini Urusi, 39 wamejeruhiwa na 28 hawajulikani walipo.

Kulingana na uchunguzi, wafanyakazi wa zamani wa kijeshi, maafisa wa zamani wa polisi na Wakenya wasio na ajira wenye umri wa miaka 20-50 ndio walengwa wakuu wa waajiri.

Waajiriwa wameahidiwa malipo ya kila mwezi ya hadi shilingi 350,000 za Kenya (dola 2,400; euro 2,000), pamoja na marupurupu kuanzia shilingi za Kenya 900,000 hadi milioni 1.2 (dola 6,200–dola 8,300; euro 5,200–euro 7,000).

Hata hivyo, wanapofika, wengi hujikuta, kulingana na taarifa zilizokusanywa, wametumwa katika mstari wa mbele wa mapigano baada ya mafunzo machache ya kijeshi.

“Wanaambiwa utafanya kazi kama mlinzi… na kufika huko na unapelekwa kwenye kambi za kijeshi,” Ichung’wah alisema.

“Umefanya mazoezi kwa wiki tatu tu. Kimsingi wanakupa bunduki tu ili ufe,” aliongeza.

Wale wanaopata mafunzo ya vilipuzi na silaha wanatakiwa kuhudhuria mafunzo kwa siku tisa tu kabla ya kutumwa kwenye mstari wa mbele, ripoti hiyo inasema.

Ichung’wah alisema kwamba, mwanzoni, waajiriwa waliondoka kupitia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Jomo Kenyatta (JKIA) wa Nairobi wakitumia visa vya watalii na kusafiri kupitia Uturuki na Falme za Kiarabu (UAE).

Hata hivyo, kutokana na ufuatiliaji mkubwa katika JKIA, wafanyabiashara hao waliripotiwa kubadilisha mbinu, wakiwaelekeza waathiriwa kupitia Afrika Kusini, Uganda na mataiafa mengine jirani.

Ripoti hiyo inabainisha baadhi ya mashirika ya kihalifu yaliyo nyuma ya kuajiri Wakenya na vituo vya matibabu vinavyotumika kwa ajili ya upimaji.

Mamlaka inasema washukiwa kadhaa, akiwemo mhusika mkuu anayedaiwa, bado wanachunguzwa kwa vitendo, huku kukamatwa zaidi kunatarajiwa. Uchunguzi unaendelea huku maafisa wakitafuta washukiwa wengine na kufanya kazi ya kuwaokoa Wakenya ambao bado wamekwama kwenye mzozo huo.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *