
Shinyanga. Watumishi wa wakala wa maji na usafi wa mazingira Vijijini (Ruwasa) mkoani Shinyanga wametakiwa kujiepusha na vitendo vya rushwa na kuhakikisha wanafanya kazi kwa weledi ili kutoa huduma bora kwa wananchi.
Angalizo hilo limetolewa leo Februari 20, 2026 na Katibu tawala Wilaya ya Shinyanga, Said Kitinga kwenye kikao kazi cha watumishi wa Ruwasa,ambapo amewataka kutumia fursa hiyo kurekebisha mapungufu yaliyopo na kuwaeleza wazi watumishi wasiowajibika.
Amesema wananchi wanahitaji kufikishiwa huduma ya maji ili kuwaondolea adha waliyokuwa wanapata na watu wakufanya kazi hiyo ni wao watumishi ili kuisaidia serikali kutimiza malengo yake ya kumtua ndoo mama kwa kusogeza huduma karibu.
“Mkatoe huduma bila ubaguzi wananchi wanachotaka ni huduma bora jiepusheni na vitendo vya rushwa fanyeni kazi kwa weledi kwani taifa linawategemea na ndiyo maana mkaaminiwa kwenye nafasi mlizonazo,”amesema Kitinga.
Katibu Tawala amesema Ruwasa wanafanya kazi kubwa kufikisha huduma ya maji Vijijini katika kuwawezesha wananchi kupata huduma bora na kuondoa malalamiko.
Amewataka kutumia kikao kazi hicho kurekebisha mapungufu yaliyopo na kuwaeleza wazi watumishi ambao wanaona hawaendi vizuri ili wasije kukwamisha jitihada za Serikali kuwapa huduma bora wananchi hasa sekta ya maji ambayo inaumuhimu mkubwa.
Kwa upande wake Meneja wa Ruwasa Wilaya ya Shinyanga Mhandisi Emmael Nkopi amesema wamejipanga vizuri kuhakikisha wanawahudumia wananchi bila upendeleo ili kuleta tija na kuondoa changamoto zote zilizopo.
Baadhi ya wafanyakazi akiwemo mhandisi Sema Sasila amesema kikao kazi kinawakutanisha wafanyakazi pamoja ili kuweza kueleza changamoto zao na kupatiwa ufumbuzi pia kupata nguvu mpya ya kufanya kazi.