Kwa mara ya kwanza baada ya wiki kadhaa, Urusi imevunja ukimya wake na kuamua kuzungumzia suala la wapiganaji wa Kiafrika katika jeshi lake nchini Ukraine. Urusi inalaani “kampeni hatari na ya kupotosha ya propaganda”, kuhusu shutuma za kupanga mitandao ya uhamiaji, udanganyifu na watu kulazimishwa kupigana katika jeshi lake nchini Ukraine, bila kukana uwepo wa wageni katika safu yake.

Imechapishwa:

Dakika 1 Wakati wa kusoma

Matangazo ya kibiashara

Na mwandishi wetu huko Moscow,

Ikitaja shutuma zilizosambaa kwa wiki kadhaa, ubalozi wa Urusi nchini Kenya unazungumzia “kampeni hatari na ya kupotosha ya propaganda” bila kutaja ni nani, kwa maoni yake, anayeandaa kampeni hii.

Inakana kabisa “kwa maneno makali” kuhusika kwa ubalozi na wafanyakazi wake katika mipango ya kuajiri watu. Pia inakana “ushirikiano wowote na vyombo au watu binafsi ambao wangewalazimisha au kuwanasa Wakenya kwa visingizio vya uongo.”

Lakini kulingana na ripoti ya kijasusi iliyowasilishwa kwa wabunge katika nchi hiyo ya Afrika Mashariki, zaidi ya Wakenya 1,000 wamesafiri kwenda Urusi na kuishia kupigana katika vita vya Urusi na Ukraine, wengi wao wakiwa hawajui hatima iliyokuwa ikiwangoja. Idadi hii ni kubwa zaidi kuliko Wakenya 200 waliotajwa hapo awali na mamlaka.

Askari wa kujitolea, kulingana na Moscow

Kwa upande mwingine, Urusi, kupitia taarifa kutoka kwa ubalozi wake, inabainisha kwamba wageni wanapigana katika safu zake. Imewaonyesha mara kwa mara kama wajitolea, kama uthibitisho kwamba haiko peke yake katika mzozo huu.

Moscow kwa muda mrefu imekuwa ikiongeza juhudi zake za kuwatia moyo wasio Warusi kupigana katika safu zake nchini Ukraine. Mapema mwezi Januari 2024, agizo la kirais la Vladimir Putin lilimpa uraia wa Urusi mpiganaji yeyote wa kigeni na familia yake baada ya mwaka mmoja wa huduma.

Hatimaye, katika taarifa yake, ubalozi umebainisha kwamba makubaliano ya pande mbili kati ya Kenya na Urusi, yaliyosubiriwa kwa miaka mingi, yanaweza kukamilishwa. Makubaliano haya yanahusu hasa uhamiaji wa wafanyakazi.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *