CHATO: HOSPITALI ya Rufaa ya Kanda Chato (CZRH) imefanikisha upasuaji wa kuondoa uvimbe wa kilogramu saba kutoka kwenye tumbo la mwanamke mmoja mwenye umri wa miaka 44.

Mwanamke huyo ambaye jina lake linahifadhiwa amekutwa na uvimbe huo kwenye sehemu ya kizazi ambapo uchunguzi umebaini ameishi nao kwa miaka minne akidhani kuwa ni ujauzito.

Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Uzazi na Wanawake CZRH, Dk Oswald Lyapa ametoa taarifa hiyo na kueleza upasuaji huo umefanyika katika kambi ya kliniki maalum ya madaktari bingwa hospitalini hapo.

Amesema mgonjwa huyo alifika hospitalini akiwa na maumivu makali ambapo awali alidhani ni ujauzito na baadaye kuhusisha na imani za kishirikina hali iliyomchelewesha kupata matibabu.

Amesema hatua hiyo ni mafanikio ya kambi ya kliniki maalumu ya madaktari bingwa inayoendelea hospitalini hapo, inayolenga kuwapatia wananchi huduma za kibingwa na ubingwa bobezi.

“Mwanamke huyu ni miongoni mwa wananchi wengi wanaoendelea kujitokeza kupata huduma katika kliniki hii, ambapo madaktari bingwa wameweka kambi hospitali ya Rufaa ya Kanda

“Matibabu haya ni sehemu ya huduma nyingi za kibingwa na ubingwa bobezi zinazotolewa na hospitali yetu kwa wananchi wote wa mikoa ya kanda ya ziwa na mikoa Jirani” amesisitiza.

Dk Lyapa ametoa wito kwa watanzania kujenga utamaduni wa kufika hospitali mapema pale wanapohisi hali ya tofauti ili kupata vipimo na matibabu kutoka kwa madaktari bingwa.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *