Wawekezaji wapatiwa leseni wakishauriwa mambo 10Wawekezaji wapatiwa leseni wakishauriwa mambo 10

WATOA huduma za uwekezaji nchini 110 wamepatiwa leseni huku wakiaswa mambo 10 ikiwemo kuwashika mkono wawekezaji wa ndani ili kutimiza maono ya Rais Samia Suluhu Hassan ya kuwa na wawekezaji wengi wa ndani.

Leseni hizo zilitolewa jana na Mkurugenzi wa Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalum ya Kiuchumi Tanzania (TISEZA), Gilead Teri wakati wa ufunguzi wa semina ya watoa huduma za uwekezaji nchini.

Alibainisha kuwa leseni hizo zitatumika ndani ya mwaka mmoja na baadaye watafanyiwa mafunzo,tathmini pamoja na uhakiki ili kupata leseni nyingine,kwamba wanafanya hivyo kwa ajili ya kuwabaini wasiokuwa waaminifu.

‘’Kuna watu wanaamini kwamba wawekezaji watu weupe tuna si Watanzani hivyo katika utoaji huduma mtoe kwa kuwavutia na kuwashika mkono wawekezaji wa ndani ili kuendana na maono ya Rais Samia ya kuwa na wawekezaji wengi wa ndani,’’alisema Teri.

Alisema wanapaswa kuwa wazalendo na kutumia ujuzi na taaluma zao kwa uaminifu ili wawekezaji wanaokuja kuwekeza nchini wakutane na watoa huduma bora.

Aliwaambia wanapaswa kuwajibika katika kutoa huduma zao na wasiruhusu nchi kupoteza sifa ya kuwa sehemu salama ya uwekezaji kwa ajili ya uvivu wao.

Teri alisema wanapaswa kufanya shughuli zao kwa kuzingatia sheria za uwekezaji na nchi,kutangaza fursa zilizopo nchini pia wanapaswa kutambua uwekezaji ni suala la kitaifa.

Alieleza kuwa jambo jingine wakati wakitekeleza majukumu yao wanapaswa kutambua kwamba uwekezaji hauwezi kufanywa na serikali pekee bali inawahitaji Watanzania na wadau wote kuungana ili kuwezesha shughuli za uwekezaji kufanyika.

Pia aliwataka kuwashawishi na kuwavutia Watanzania kuwekeza katika biashara ya mali isiyohamishika,waepuke kuomba au kupokea rushwa bali wafanye kazi kwa kuzingatia taaluma zao.

Alisema hawapaswi kubaki kuwa watoa huduma tu bali na wanapaswa kuwa wawekezaji kabla ya kuwavutia wengine kuwekeza nchini kwa sababu uwekezaji si kuwa na mtaji mkubwa wanaweza wakaanza wakiwa na mtaji mdogo.

Alieleza kwamba walikutana na watoa huduma kuwarasimisha ili washirikiane nao zaidi na kuhakikisha wanalinda uweledi katika eneo la kuwahudumia wawekezaji pamoja na kuhakikisha huduma zinazokwenda kwa wawekezaji zinaleta taswira njema ya nchi pamoja na kuwaondoa matapeli.

Alibainisha kuwa wamefanya hivyo kwa sababu wawekezaji wengi wakija nchi kuwekeza wanatumia kada mbalimbali za watoa huduma nchini ikiwemo wanasheria,watu wanawasaidia kutafuta ardhi,ulipaji wa kodi na masuala ya uhasibu.

‘’Tunawafundisha namna ya kutoa huduma kwa wawekezaji ili kuepuka wawekezaji kutumia watu wasiokuwa rasmi ambao mwisho wa siku wanachafua taswira ya Tanzania kuwa sehemu salama ya uwekezaji,tunawaona kama wadau muhimu ndio maana tumewaleta kwenye wigo mmoja ili kuwasaidia katika utendaji wao wa kazi ili kusogeza mbele gurudumu la uwekezaji nchini,’’alisema.

Alisema asilimia 100 ya waliopatiwa leseni hizo ni Watanzania hivyo wanatumia fursa hiyo kama sehemu ya kuwaelimisha Watanzania fursa za uwekezaji nchini ili kuwafikia wawekezaji wa ndani wengi zaidi.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *