
Dar es Salaam. Wakati Serikali ikifanya jitihada za kurudisha umoja wa kitaifa baada ya matukio ya Oktoba 29, 2025, mwanasiasa mkongwe, Dk Wilbrod Slaa amesema taifa haliwezi kuendelea na mchakato wa maridhiano wala Katiba mpya wakati suala la mauaji halijapatiwa ufumbuzi.
Amesema kuzungumzia maridhiano au Katiba mpya wakati huu ambapo bado kuna watu hawajui kama ndugu zao wamefariki dunia au la, ni ubinafsi wa kutaka kujinufaisha kisiasa na hilo haliwezekani.
Dk Slaa amebainisha hayo kwenye mahojiano maalumu na Mwananchi hivi karibuni, akizungumzia masuala mbalimbali ikiwamo mchakato wa maridhiano baada ya mauaji ya Oktoba 29, 2025 pamoja na Katiba mpya.
Tayari Rais Samia Suluhu Hassan ameunda Tume ya Kuchunguza Matukio Wakati na Baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025, inayoongozwa na Jaji Mkuu mstaafu, Mohamed Chande Othman, ambayo mapendekezo yake ndiyo yatatoa mwongozo kuelekea kwenye maridhiano.
Tume hiyo inaendelea kusikiliza maoni ya wadau mbalimbali ili kujua chanzo cha yaliyotokea siku ya uchaguzi na kisha kutoa mapendekezo ambayo kwa mujibu wa Rais Samia, ndiyo yatachonga njia kuelekea kwenye maridhiano na kuandika Katiba mpya.
Katika hotuba yake wakati akizindua Bunge la 13, Rais Samia alisisitiza kwamba hatachoka kunyoosha tena mkono wa maridhiano na ni matumaini yake kuwa wadau wa kisiasa wataupokea kwa dhati mkono huo kupitia Tume hiyo ili kujenga mwafaka wa kitaifa.
Katika mahojiano hayo, Dk Slaa amesema ni jambo lisilowezekana kuzungumza maridhiano au Katiba mpya wakati watu wana maumivu, watu hawajazika wapendwa wao na wengine hawajui kama watu wao wako hai au wamekufa.
“Hatuwezi kuzungumza maridhiano hatujui maiti za ndugu zetu ziko wapi, tuzipate maiti tuzipumzishe, baada ya hapo ndiko tunaweza kuzungumzia maridhiano na hiyo ndiyo siasa ninayoijua na niliyofundishwa,” amesema.
Katibu Mkuu huyo wa zamani wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), amesema uelewa wake kwenye siasa si wa kuokotwa, bali amesomea, hivyo hawezi kuzungumzia chochote kabla ya watu kupata ndugu zao.
Kama hilo haliwezekani, Dk Slaa amesema ni vema mamlaka zikatoka na kutoa tamko rasmi kwamba hakuna waliopoteza maisha na maiti zilizoonekana zilipelekwa wapi.
“Ninachojua mtu akifariki dunia, ndugu zake wanapewa mwili, sasa kipindi hiki watu bado wamechanganyikiwa, hawawaoni ndugu zao, unasema maridhiano. Hatuwezi kusema kuna maridhiano, ni jambo la ajabu kuzungumzia hayo wakati hatujui ndugu zetu wako wapi, hatuna sehemu nyingine za kuzungumzia mambo hayo.
“Kuna wanaosema Katiba mpya, hatuwezi kutaja Katiba sasa wakati hatujazika ndugu zetu, anayesema maridhiano sasa anaangalia masilahi yake ya kisiasa, hili haliwezekani, maridhiano ni siasa,” amesema mwanasiasa huyo.
Yanayoendelea Chadema
Kuhusu halki ya Chadema Dk Slaa amesema hakuna asiyejua kinachoendelea ndani ya chama hicho, akidai ni njama za kisiasa za kukididimiza chama hicho cha upinzani kupitia zuio la chama hicho kutofanya siasa kufuatia kesi iliyofunguliwa dhidi yake.
Chadema inakabiliwa na kesi ya madai inayohusiana na mgogoro wa madai ya mgawanyo wa rasilimali za chama usio sawa kati ya Bara na Zanzibar iliyofunguliwa na baadhi ya wajumbe wa Bodi ya Wadhamini kutoka Zanzibar.
Kesi hiyo ya madai namba 8323 ya mwaka 2025 ilifunguliwa na Makamu Mwenyekiti mstaafu wa Chadema, Said Issa Mohamed na wajumbe wawili wa Bodi ya Wadhamini wa Chadema kutoka Zanzibar, Ahmed Rashid Khamis na Maulida Anna Komu.
Hivi karibuni, viongozi wa Chadema wametoa maelekezo kwa viongozi wa ngazi za chini wakiwaelekeza kuanza kutumia ofisi na mali za chama hicho wakidai zuio lililokuwa limewekwa limekwisha muda wake.
Akizungumzia suala hilo, Dk Slaa amebainisha kwamba sarakasi zote zinazochezwa dhidi ya Chadema si za kweli, zina lengo la kukidhoofisha chama hicho kwa kuwa kinasimamia misingi ya demokrasia na maendeleo ya taifa.
“Hakuna asiyejua kuwa suala la Chadema kufungiwa kufanya siasa sio sahihi na pale hakuna mgogoro wa mgawanyo wa mali, kwa bahati nzuri wanachosema sasa, wakati huo nilikuwa Katibu Mkuu, kwa hiyo uongozi wa sasa haupaswi kuwa na mgogoro.
“Kama wanataka waachie chama tufike mwisho haki ipatikane, sio kuzuia chama kufanya siasa kwa hila,” amesema Dk Slaa ambaye aliwahi kuwa Balozi wa Tanzania nchini Sweden kabla ya kuvuliwa hadhi ya ubalozi mwaka 2023.
Dk Slaa amesisitiza kwamba yupo tayari kwenda kutoa ushahidi wowote utakaohitajika kwa kuwa mgawanyo wa mali una utaratibu wake.
Amesema aliyeishtaki Chadema kudai mgawanyo wa mali sasa, ndiye aliyekuwa na mamlaka za kugawa mali hizo (mama Anna Komu), jambo analodai ndiyo sababu ya kesi hiyo kutafsiriwa kama ya kutengeneza.
“Said Mohamed alikuwa mwenyekiti wa hiyo kamati na Komu naye alikuwepo, watu wa kushitakiwa walikuwa ni wao. Kama ingebainika dosari, mwenyekiti wa sasa, Tundu Lissu alishika uongozi hivi karibuni, sasa waligawa mali lini, waliogawa ndio wanaleta kesi hii, inawezekanaje?” amehoji.
Hata hivyo, Dk Slaa amesema yote hayo ambayo Chadema inayapitia hayawezi kuidhoofisha bali chama hicho kinaendelea kuimarika zaidi.
“Hiki wanachofanyiwa Chadema ni mkakati bandia, kinachoendelea ni kinyume na Katiba, tumeshalalamika kilichofanywa na Msajili wa Vyama vya Siasa si sahihi,” amesema mwanasiasa huyo.
Ni chama makini
Mgombea huyo wa urais wa Chadema mwaka 2010, amesema licha ya kuwa Tanzania kuna vyama vya upinzani zaidi ya 10, ameiona Chadema pekee ndicho chama makini.
“Nilishasema kabla ya kuingia kwenye uchaguzi, hakuna uchaguzi na tunapoteza fedha kwa kuwa hatukuwa na vyama vya siasa. Niliviambia hivyo vyama, wanatupotezea fedha zetu,” amesema Dk Slaa.
Mwanasiasa huyo mkongwe aliyewahi kuwa mbunge wa Karatu (Chadema) kati ya mwaka 1995 – 2010, amesema yeye ni mwanachama wa chadema na hakuwahi kuondoka ndani ya chama hicho, licha ya kuteuliwa kuwa balozi.
Dk Slaa ambaye wakati huo alikuwa akiishi Canada baada ya kujitenga na siasa, alitangaza uamuzi huo baada ya chama hicho kumpokea Edward Lowassa kama mgombea urais wa Chadema.
Amesema ukimya wake wakati huo ulisababishwa na kazi ya muda aliyopewa, lakini hakuondoka Chadema.
“Nimerudi kuwa mwanachama, mimi ni mzee wa Chadema hadi sasa wananitumia kama ulivyoona kwenye kampeni ya ‘No Reforms No Election’ (bila mabadiliko, hakuna uchaguzi) na sina kikwazo kutumiwa maana chama kipo kwa mujibu wa sheria,” amesema Dk Slaa.