MOROGORO: JUMLA ya vijana 42,000  wamenufaika na programu za muda mrefu na muda mfupi kwa kupatiwa elimu na mafunzo ya ufundi stadi kupitia Mradi wa Mpango wa Elimu Changamani kwa Vijana Walio nje ya Shule (IPOSA) unaotekelezwa Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima (TEWW).

Mpango huo unalenga makundi mahsusi ya vijana ambao hawakuwahi kwenda shule, walioacha shule katika ngazi ya msingi, sekondari, waliomaliza darasa la saba na hawakupata fursa ya kuendelea na elimu ya sekondari.

Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi wa Taasisi hiyo, Profesa Philipo Sanga amesema hayo wakati akimkaribisha Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dk Hussein Mohamed Omar kufungua mkutano wa 16 wa Baraza la Wafanyakazi wa Taasisi hiyo .

Naibu Katibu mkuu huyo, hotuba yake iliyosomwa kwa niaba yake na Mkurugenzi wa Elimu Msingi wa wizara hiyo, Abdul Maulid.

Profesa Sanga ambaye pia ni Mkuu wa Taasisi hiyo amesema kupitia mradi huo  vijana 12,000 wamenufaika na programu za muda mrefu ambapo wavulana ni   5,406  na wasichana 6,594 na wengine 30,183  wakinufaika na program ya  muda mfupi kwa kupatiwa  elimu na mafunzo ya ufundi stadi.

Amesema kupitia mradi huo, Taasisi ilifanikiwa  kupata fedha kiasi cha USD 400,000 kwa ajili ya ujenzi wa karakana tatu za mfano.

Profesa Sanga amesema karakana moja imejengwa mkoa wa Manyara na imekamilisha ujenzi kwa asilimia  99  na kazi iliyobaki ni ya kuweka milango na madirisha pekee na nyingine mkoa wa Shinyanga  ujenzi umefikia asilimia 70 , wakati Tanga umefikia  asilimia 75.

Amesema karakana hizo zitaendelea kuwasaidia vijana  walio nje ya mfumo rasmi wa shule kupata ujuzi wa mafunzo ya ufundi, Stadi za Maisha, Ujasiriamali na Stadi za Kusoma, Kuandika na Kuhesabu (KKK).

Katika  mradi wa Kuimarisha Ubora wa Elimu ya Sekondari kwa njia mbadala nchini (SEQUIP-AEP).ulianza kutekelezwa  mwaka 2022  kufikia ukomo mwaka huu (2026) alisema  hadi 2025, jumla ya wasichana 13,272  walisajiliwa.

Profesa Sanga amesema wasichana hayo ni waliokuwa wamekatiza masomo ya sekondari  na kuendelea na masomo na hivyol kuvuka lengo kwa  asilimia 111 ya kusajili wasichana 12,000 kulingana na agizo la Serikali hadi  kufikia mwaka   2026

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu huyo kwenye  hotuba hiyo aliipongeza Taasisi kwa kuimarisha ushirikishwaji wa wafanyakazi na kuonesha mafanikio katika utekelezaji wa miradi hii ya  kimkakati.

Pia ameitaka kusimamia kwa karibu miradi  hiyo ili kuhakikisha rasilimali za umma zinatumika kwa uwazi na kutoa matokeo yanayopimika.

“Wizara inawapongezeni kwa kuimarisha ushirikishwaji wa wafanyakazi kupitia Baraza la Wafanyakazi na kuonesha mafanikio katika utekelezaji wa miradi hii ya  kimkakati,” amesema Dk Omar.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *