Ukoloni katika karne ya 19 na 20 haukuwa tu ukihusiana na kueneza bendera katika ramani ya dunia; bali ulikuwa mradi uliopangwa wa kutwaa ardhi, rasilimali, na nguvukazi ambao ulibadilisha miundo ya kiuchumi na kijamii ya watu waliokuwa chini ya ukoloni.

Katika mfumo huu usio sawa, makoloni yakawa wasambazaji wa malighafi na masoko ya watumiaji, na mifumo ya wenyeji ilibadilishwa na uzalishaji unaolenga mauzo ya nje, mchakato ambao mara nyingi uliambatana na kazi za lazima, kodi, ukandamizaji na njaa iliyoratibiwa. Ujerumani, ambayo iliingia katika ushindani wa kikoloni baadaye kuliko mataifa mengine ya Ulaya, ilitekeleza mojawapo ya mifano ya kikatili zaidi ya mfumo huu katika eneo la Afrika Mashariki.

Mwishoni mwa karne ya kumi na tisa, utawala mpya ya Ujerumani iliyoungana uliingia katika mbio za kikoloni baadaye kuliko mamlaka zingine za Ulaya, lakini ulipoingia, ulichukua hatua kwa kasi na vurugu. Katika koloni linalojulikana kama Afrika Mashariki ya Kijerumani (German East Africa), ukoloni haukuwa tu na fasili na maana ya utawala wa kisiasa; lakini pia ulimaanisha marekebisho ya kulazimishwa ya uchumi, kubadilisha muundo wa umiliki wa ardhi, kulazimisha mazao ya kuuza nje, na hatimaye kubadilisha kilimo cha asili kuwa mkono wa sekta ya Ulaya. Kilichotokea katika ardhi hii kilikuwa mfano bayana wa “ukoloni wa kilimo”; utaratibu ambao ardhi, nguvukazi, na mazao vilipangwa si kulingana na mahitaji ya kujikimu ya jamii ya wenyeji bali kulingana na maslahi ya viwanda ya jiji kuu. Uzoefu huu haukuwa tu kipindi cha utawala wa kikoloni, bali maabara ya kutumia nguvu kupitia njaa, moto, na kazi za kulazimishwa.

Katika miaka ya 1880, Ujerumani iliimarisha udhibiti wake Afrika Mashariki kupitia makampuni ya kikoloni na kisha kupitia uingiliaji wa moja kwa moja wa serikali. Muundo huu ulitegemea nguzo tatu: Kodi ya kila mtu, kazi za kulazimishwa, na upangaji wa vikosi vya wenyeji vilivyoitwa “Askari” (askari wenyeji) chini ya amri ya maafisa wa Ujerumani. Lengo lilikuwa kubadilisha eneo hilo kuwa uchumi unaolenga mauzo ya nje ili kusambaza malighafi kwa ajili ya viwanda vya Ujerumani, hasa kusokota nyuzi na kufuma nguo.

Katika muktadha huu, zao muhimu zaidi lilikuwa pamba, zao ambalo halikuwa muhimu kwa kulisha wakazi wa eneo hilo bali kwa viwanda vya nguo vya Ulaya. Viwanda vilivyoinukia vya Ujerumani vilihitaji pamba mbichi na ya bei nafuu, na kwa kuwa sehemu kubwa ya biashara ya pamba duniani ilikuwa mikononi mwa Uingereza na Marekani, serikali ya Ujerumani ilijaribu kupunguza utegemezi wake kwao kwa kuizalisha katika makoloni yake na kuchukua udhibiti wa moja kwa moja wa vyanzo vya malighafi. Matokeo yake, kilimo cha ndani kililazimika kulima pamba badala ya mtama, mahindi, mihogo, na mazao mengine ya chakula. Hatua hii ilipelekea kuvurugika kwa usawa na mlingano wa kitamaduni kati ya uzalishaji na matumizi ya ndani.

Kinjekitile Ngwale, shujaa wa vita vya majimaji

Kuanzia mwanzoni mwa karne ya 20, serikali ya Ujerumani huko Tanganyika ambayo baadaye ilikuja kuungana na Zanzibar na kuzaliwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ilitekeleza mpango wa kilimo cha pamba cha lazima. Vijiji vilihitajika kuzalisha mgao fulani wa pamba kwa ajili ya kuuza nje, hata katika maeneo ambayo hali ya hewa na rasilimali za maji hazikufaa kwa zao hilo. Sera hii iliwatenganisha wakulima na kulima mazao ya msingi ya chakula, ikiwalazimisha kujitolea ardhi na nguvukazi yao kwa mazao ambayo hayakutoa chakula na yalikusudiwa kwa ajili ya masoko ya Ulaya pekee.

Katika miaka iliyofuata, sera hizi zilitekelezwa kwa nguvu na usimamizi mkubwa zaidi, na mfumo wa mgao ukaenea. Matokeo yake yalikuwa ni kupungua uzalishaji wa chakula na akiba ya nafaka na kuongezeka kwa hatari ya ukame; kwa njia ambayo usalama wa chakula wa jamii ulidhoofika na mfumo wa kujipatia riziki uliporomoka polepole. Kadiri ukame na uhaba wa chakula ulivyozidi kuongezeka, ndivyo hali ilivyozidi kuwa mbaya na kutoridhika kulienea si tu katika ngazi ya kiuchumi, bali pia katika ngazi za kijamii na kitamaduni.

Mazingira haya yaliandaa uwanja wa kuibuka na kuenea upinzani. Katika kiangazi cha 1905, shinikizo la kiuchumi na kijamii lilifikia hatua ya kuripuka, na uasi wa kitaifa dhidi ya utawala wa kikoloni wa Ujerumani ulianza, ambao baadaye ulijulikana kama Uasi wa Maji Maji. Mnamo tarehe 20 Julai 1905, wapiganaji Wamatumbi waliharibu mashamba ya pamba ambayo yalikuwa nembo ya unyonyaji wa kiuchumi, na kufanya cheche za uasi kuenea.

Uasi huo ulichochewa na uongozi wa kiroho wa Kinjekitile Ngwale, lakini mizizi halisi ya uasi huo ilitokana na miaka mingi ya shinikizo la kiuchumi, kodi, na udhalilishaji.

Wanajeshi wa kikoloni wa Ujerumani kwenye Reli ya Tanganyika jijini Dar es Salaam, mwanzoni mwa karne ya 20.

Jibu la Wajerumani kwa uasi huo halikuwa la kijeshi tu, bali pia la kujikimu, kwani vikosi vya Wajerumani na askari vilitekeleza sera ya “ardhi iliyoungua”: Kuchoma vijiji, kuchoma maghala, kuharibu mifugo, na kuharibu visima vya maji. Lengo lilikuwa ni kukata usambazaji wa chakula na kuwabakisha watu na njaa ili wajisalimishe. Matokeo yake yalikuwa njaa iliyoenea, inayojulikana kama “Njaa Kubwa.” Makadirio yanaweka idadi ya waathiriwa kati ya 75,000 na 300,000; wengi wao walikufa si kwenye uwanja wa vita, bali kutokana na njaa na magonjwa.

Vita vya Majimaji halikuwa tukio la kwanza la ukandamizaji wa kikatili wa Wajerumani. Hapo awali, katika Vita vya Abushiri wa 1888–89, upinzani wa pwani ulikuwa umekandamizwa kwa nguvu, na sera kama hizo za adhabu zilitekelezwa baada ya kushindwa Wahehe chini ya chifu Mkwawa katika miaka ya 1890.

Hatua za Ujerumani katika Ukanda wa Afrika Mashariki si hadithi tu ya uasi ulioshindwa; bali ni simulizi ya utaratibu wa kiuchumi uliobadilisha ardhi kuwa nguzo ya kuuza bidhaa nje, mashamba kuwa shabaha ya kijeshi, na chakula kuwa chombo cha vita. Kumbukumbu ya kihistoria ya watu wa eneo hilo inakumbukwa kwa miaka mingi ambapo mashamba yalichomwa moto, maghala ya chakula yalibakia matupu, na ukame na njaa vikienea; urithi mzito ambao bado umegubika kwa kivuli historia ya Afrika Mashariki.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *