
Arusha. Wakurugenzi wa usimamizi wa mifumo ya Benki Kuu pamoja na wanaosimamia uangalizi wa vihatarishi na muunganiko wa mifumo kutoka nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara (SADC), wanakutana jijini Arusha kwa siku tano kujadili vihatarishi vya mifumo ya kibenki, udukuzi wa mifumo ya fedha na kasi ya ukuaji wa teknolojia.
Hayo yamesemwa leo, Jumatatu Februari 23, 2026, na Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Emmanuel Tutuba, wakati wa ufunguzi wa mkutano wa 33 wa Kamati Ndogo ya Tehama na Usimamizi wa Vihatarishi vya Benki Kuu za nchi wanachama wa SADC.
Amesema mkutano huo utachambua vihatarishi vinavyoweza kuathiri utekelezaji wa shughuli za kiuchumi na kibenki, ikiwemo udukuzi wa mifumo ya fedha na matumizi ya fedha za mtandao.
“Ni muhimu kuangalia vihatarishi vya mifumo ya kibenki na teknolojia mpya ili kuhakikisha miamala inafanyika bila kukwama. Kukwama kwa miamala kunaweza kusababisha hasara na kuondoa imani ya wadau wa sekta ya fedha,” amesema.
Mkutano huo umewashirikisha wajumbe 57 kutoka nchi 16 za Sadc, na mapendekezo yake yatawasilishwa kwa Kamati ya Magavana wa Benki Kuu (CCBG) wa nchi wanachama.
Tutuba amesema teknolojia mpya zinazoingia kwenye sekta ya fedha huleta fursa na changamoto, hivyo wataalamu wanatarajiwa kuweka mikakati ya pamoja ya kuimarisha biashara na uhawilishaji wa fedha kati ya nchi wanachama.
Akizungumzia hali ya uchumi wa Tanzania, amesema kwa mwaka uliopita ulikua kwa wastani wa asilimia sita, huku mfumuko wa bei ukidhibitiwa katika wastani wa asilimia 3.3.
“Hii inaonyesha mifumo mizuri ya usimamizi wa uchumi. Mfumuko wa bei unapokuwa chini huongeza imani ya wawekezaji na kulinda thamani ya fedha,” amesema.
Awali, Mkurugenzi wa Usimamizi wa Mifumo ya Tehama BoT, Michael Mtweve, amesema mkutano huo unawakutanisha wakurugenzi wa mifumo na vihatarishi kujadili ushirikiano katika kuimarisha mifumo ya benki na kukabiliana na teknolojia mpya.
Amesema miongoni mwa masuala yatakayojadiliwa ni matumizi ya Akili Mnemba (AI) na vihatarishi vinavyoweza kuambatana nayo.
“AI inaweza kurahisisha utendaji kazi lakini pia inaweza kutumiwa vibaya na wahalifu kama haitasimamiwa vizuri. Tunahitaji mikakati madhubuti ya kuipokea na kuilinda mifumo yetu,” amesema.